“Shahidi Aliye Mbinguni Mwaminifu”
KWA muda mrefu kabla ya mwanadamu wa kwanza kuitembea dunia, mwezi umeng’aa kwa wangavu katika anga ya usiku. Wakati mmoja wengi waliuabudu kuwa kijimungu-kike. Mtungaji vitabu Mgiriki Plutarch alidai kwamba mwezi ulikuwa kituo cha mwisho cha nafsi safi baada ya kifo. Katika ngano ya Kibaltiki mwezi ulikuwa mwanamume, mume wa jua. Walikuwa na gombano la ndoa, na mwezi ukamtoroka mke wao, usitokee mara nyingi pamoja naye mbinguni!
Leo, wapenzi vijana—na wasio vijana sana—huutazama mwezi na kufikiria mawazo ya kimahaba. Katika miaka ya 1960 wanasayansi walitumia hesabu kubwa mno za pesa kuwapeleka watu kwenye mwezi ili warudi na ratili chache za miamba kwa ajili ya utafiti. Jambo moja kuhusu mwezi ni la hakika. Kila siku, kwa wakati barabara utachomoza na kutua. Ni mwaminifu sana katika mizunguko yao hivi kwamba twaweza kuhesabu umetokea mara ngapi na kupatwa mara ngapi hadi maelfu ya miaka ambayo imepita.
Waisraeli walipoutazama mwezi, walikumbushwa juu ya jambo fulani la ajabu. Mungu aliahidi kwamba utawala wa kifalme wa Mfalme Daudi usingepitilia mbali. Alisema hivi: “[Mbegu ya Daudi] [i]tathibitika milele kama mwezi; shahidi aliye mbinguni mwaminifu.” (Zaburi 89:35-37) Ahadi hiyo ilitimizwa katika Yesu, “Mwana wa Daudi.” (Luka 18:38) Baada ya kifo chake Yesu alifufuliwa akiwa roho asiyeweza kufa akapaa mbinguni. (Matendo 2:34-36) Baadaye aliwekwa kuwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu wa kimbingu. (Ufunuo 12:10) Ufalme huo unatawala sasa nao “utasimama milele na milele.” (Danieli 2:44) Katika njia hiyo Yesu, mwakilishi asiyeweza kufa wa utawala wa kifalme wa Daudi, atadumu muda mrefu kama mwezi, “shahidi aliye mbinguni mwaminifu.”
Kwa hiyo, kila wakati unapouona mwezi uking’aa kwa wangavu katika anga ya usiku, kumbuka ahadi ya Mungu kwa Daudi na utoe shukrani kwamba Ufalme wa Mungu unatawala sasa na utatawala milele, kwa utukufu wa Mungu na kwa baraka ya milele ya ainabinadamu yenye uaminifu.—Ufunuo 11:15.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]
Frank Zullo