Utiaji-Damu Mishipani Wasifiwa Kupita Kiasi?
Utiaji-damu mishipani ni jambo la kawaida katika utibabu wa ki-siku-hizi, lakini je, wastahili kusifiwa sana? Wewe wafikirije?
Katika jarida The American Journal of Medicine (Februari 1993), Dakt. Craig S. Kitchens aliuliza hivi: “Je! utiaji-damu mishipani wasifiwa kupita kiasi?” Alionyesha kwamba mara nyingi matabibu huchunguza kwa uangalifu kama manufaa za utibabu fulani zazidi hatari ambazo huenda utibabu huo ukasababisha. Namna gani utiaji-damu mishipani?
Kitchens alipitia uthibitisho wa hivi karibuni wa hatari nyingi zinazohusiana na utiaji-damu mishipani, kama vile mchochota wa ini, mfumo wa kinga uliokinzwa, kushindwa kwa mfumo wa kiungo fulani, na maitikio yanayohusu kinga. Uchunguzi mmoja uliokuwa ukitoa muhtasari wa “matatizo mengi mno” yanayotokana na utiaji-damu mishipani “ulikata maneno kwamba kila utiaji-damu mishipani unaofanywa una uwezekano wa ujumla wa kuwa na matokeo mabaya wa asilimia 20, baadhi yayo ni madogo lakini mengine ni yenye kudhuru,” hata yenye kusababisha kifo.
Hata hivyo, je, hatari hizo zastahili kukabiliwa kwa sababu ya zile zinazodhaniwa kuwa manufaa za utiaji-damu mishipani?
Dakt. Kitchens alipitia uchunguzi 16 ulioripotiwa wenye kuhusisha upasuaji wa visa 1,404 waliofanyiwa Mashahidi wa Yehova, wanaokataa utiaji-damu mishipani kwa kutii amri ya Biblia ya ‘kujiepusha na damu.’—Matendo 15:28, 29.
Tokeo lilikuwa nini? “Ule uamuzi wa wagonjwa walio Mashahidi wa Yehova wa kuepuka utiaji-damu mishipani katika taratibu za upasuaji mkuu waonekana kuongeza uwezekano wa kifo wa asilimia 0.5 hadi asilimia 1.5 kwenye hatari za upasuaji kwa ujumla. Isiyojulikana kwa wazi hata zaidi ni kadiri ya ugonjwa na kifo inayoepukwa na zoea hilo, lakini labda [kadiri hiyo ya ugonjwa na kifo inayoepukwa] inapita kiasi cha hatari za kutotiwa damu mishipani.” (Italiki ni zetu.) Alionyesha nini? Labda hatari zozote za kitiba zinazotokana na kukataa damu ni chache kuliko hatari zinazohusika katika kukubali utiaji-damu mishipani.
Kwa hiyo, swali la Kitchens linalostahili kuulizwa ni: “Ikiwa kutowatia Mashahidi wa Yehova damu mishipani hutokeza hasa ongezeko kidogo zaidi la ugonjwa na kifo cha ghafula na huepuka kiasi kikubwa sana cha gharama na matatizo yenye kusedeka, je, wagonjwa watiwe damu mishipani kidogo zaidi?”
Wale wanaokataa utiaji-damu mishipani kwa msingi wa uthibitisho huo watakuwa pia wakitenda kulingana na mielekezo kutoka kwa Muumba wetu.