Hasira Yangu au Afya Yangu?
NI NANI ambaye hakasiriki? Hilo hutupata sote. Nyakati nyingine kadiri fulani ya hasira yaweza kuwa ya haki. Lakini, kwa haki, je, si kweli kwamba mara nyingi hasira yetu (au kiasi chayo) si ya haki?
Biblia hutuambia hivi: “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu, usikasirike, mwisho wake ni kutenda mabaya.” (Zaburi 37:8) Shauri hilo ni lenye hekima kadiri gani? Je! lingeweza kuathiri afya yako kwa muda mrefu?
Katika sehemu yalo ya “Afya,” The New York Times lilisema hivi:
“Watu ambao mara nyingi huwaka kwa hasira kali au ambao hukaa wakiwa wameghadhabika juu ya kila jambo dogo ambalo wameona kuwa udhia waweza kuwa wanasababisha mengi kuliko kufanya wenyewe wasiwe watu wenye kupendeza. Waweza kuwa wanajiua wenyewe.
“Watafiti wamekusanya habari nyingi hivi karibuni inayodokeza kwamba hasira nyendelevu huudhuru mwili sana hivi kwamba hiyo hulingana na, au hata hupita, uvutaji wa sigareti, unene wa kupita kiasi na ulaji unaotia ndani mafuta mengi, ikiwa sababu kubwa ya kifo cha mapema.
“‘Uchunguzi wetu mbalimbali waonyesha kwamba hasira yenye kushuku, iliyo na uhasama yalingana na hatari nyingine yoyote kwa afya ambayo twajua juu yayo,’ akasema Dakt. Redford Williams, mtafiti katika tiba inayohusu mwenendo kwenye Kitovu cha Kitiba cha Chuo Kikuu cha Duke.”
Uchunguzi mbalimbali waonyesha kwamba wale ambao huitikia matatizo ya kila siku maishani kwa njia ya kupita kiasi hutokeza hormoni nyingi zaidi za mkazo wa akili. Kuwaka kwao mara kwa mara kwaweza kusababisha ukosefu wa usawaziko kati ya ule unamna-namna wa kolesteroli wenye kulinda na ule wenye kudhuru, hivyo wakiwa na hatari ya kupatwa na maradhi ya mishipa ya moyo.
Huenda wengine wakaitikia hivi, ‘Lakini ndivyo mimi nilivyo tu’ au, ‘Ndivyo nilivyokua.’ Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba huwezi kubadilika, kwa kujaribu kutumia shauri la Mungu kwa moyo mweupe. Katika Biblia yako mwenyewe, chunguza shauri lake juu ya hasira na ghadhabu lililorekodiwa kwenye Mithali 14:29, 30; 22:24, 25; Waefeso 4:26; Yakobo 1:19, 20.
Kutumia hekima hiyo ya kimungu kwaweza kuboresha afya yako na kurefusha uhai wako. Gazeti Times lilisema hivi: “Watafiti wengi walisema kwamba watu wanaoelekea kukasirika wangeweza kupunguza hatari ya kifo cha mapema kwa kubadili maitikio ya haraka, yenye uhasama.”