Je! Yaweza Kukunufaisha?
GAZETI ulilo nalo mkononi limekusudiwa kuwa chanzo cha kitia-moyo, likikumbusha miongozo ya Biblia ya kuimarisha familia na kudumisha uaminifu-maadili wa kibinafsi. Hilo huonyesha kwamba nyakati za leo zenye matatizo zilikuwa zimetabiriwa katika Biblia, na hukazia suluhisho—Ufalme wa Mungu. Je! waweza kunufaishwa na Mnara wa Mlinzi na, Amkeni!, gazeti-jenzilo?
Kutoka Ufilipino mwanamke mmoja aitwaye Vilma aliandika hivi: “Ikiwa kuna maneno yoyote ya kufafanua vichapo vyenu, nadhani ningeteua [maneno] ‘ni mazuri ajabu.’ Niliona na kusoma kwa mara ya kwanza [magazeti yenu] Amkeni! na Mnara wa Mlinzi nilipokuwa kwenye basi nikirudi nyumbani kutoka Manila. Kwa kawaida mimi huchukua magazeti ya habari ninaposafiri, lakini wakati huu sikuchukua yoyote.
“Mtu mmoja wa makamo aliyekuwa ameketi kando yangu katika safari hiyo alikuwa na vichapo vyenu. Baada ya yeye kusoma Amkeni!, alitoa gazeti jingine, Mnara wa Mlinzi. Nilitwaa fursa hiyo kuazima Amkeni! Kwa kweli kabisa, nilifurahia sana kuyasoma magazeti hayo kwa sababu makala zote zilipendeza, zilikuwa za wakati ufaao, na zenye kujenga.”
Mwanamke huyo alimalizia hivi: “Nataka kuyapokea magazeti yenu. Tafadhali nijulisheni jinsi niwezavyo kuyapokea.” Ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika Ufilipino ilifurahia kusaidia kwa kuongeza jina la mwanamke huyo kwenye orodha yayo ya kupeleka magazeti kwa posta.