Kwenda Mbinguni au Helo?
“KUNA uwezekano gani kwamba wewe utakwenda mbinguni au helo”?
Kwa msingi, Waamerika mbalimbali waliulizwa hilo katika uchunguzi mmoja uliofanywa hivi karibuni. Kitovu cha Utafiti wa Dini cha Princeton kilitangaza kwa chapa matokeo katika Religion in America 1992-1993.
Wewe ungalijibuje? Kuna uwezekano gani kwamba mwenzi wako wa ndoa au wapendwa wako wengine watakwenda mbinguni wanapokufa? Je! wafikiri yawezekana kwamba wewe, au wao huenda wakaenda helo hatimaye?
Uchunguzi huo ulionyesha kwamba asilimia 78 walifikiri kwamba uwekezano wao wa kwenda mbinguni ulikuwa mzuri au bora kabisa, zaidi ya idadi ya wale waliojibu hivyo karibu miaka 40 iliyopita. Helo? Karibu asilimia 77 walisema uwezekano wa kwenda huko ulikuwa mdogo.
Je! majibu yao yalitegemea ujuzi sahihi wa Biblia? Karibu 4 kati ya 10 walikiri kuhudhuria mahubiri ya kidini mara chache zaidi ya vile walivyofanya miaka mitano iliyopita. Ni asilimia 28 pekee waliodai kushiriki katika vikundi vya funzo la Biblia na asilimia 27 katika masomo ya elimu ya kidini.
Ukijifunza Biblia kwa uangalifu, utapata mambo kadhaa yenye kushangaza. Kwa kielelezo, Biblia husema kwa wazi kwamba wakati wa kifo Yesu alikwenda “helo,” kama ilivyofasiriwa katika tafsiri fulani za Biblia. (Matendo 2:31, King James Version; “Hadesi,” NW) Neno la Mungu lathibitisha pia kwamba wala Mfalme Daudi wala Yohana Mbatizaji hawakwenda mbinguni walipokufa. (Mathayo 11:11; Matendo 2:29) Hayo ni mambo ya hakika, si maoni tu kutoka kwa uchunguzi wa kidini.
Mambo mengine ya hakika ambayo huenda yakakuathiri: Biblia hufundisha kwamba mitume wa Yesu na idadi ndogo ya wengine watachukuliwa mbinguni ili kutawala pamoja na Yesu. Hata hivyo, watu walio wengi ambao wamekufa walikwenda tu kwenye kaburi la kawaida la ainabinadamu. Mungu atawafufua, akiwaleta kwenye uhai duniani wakiwa na taraja la uhai kamili, wenye furaha, usio na kikomo katika paradiso ya kidunia iliyorudishwa.
Mashahidi wa Yehova wangefurahia kukusaidia kuthibitisha kutoka katika Biblia yako mwenyewe msingi wenye kutegemeka wa tumaini hilo.