“Kama Siku za Mti”
ZAIDI ya miaka elfu tatu iliyopita, Musa aliandika hivi: “Siku za miaka yetu ni miaka sabini, na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; na kiburi chake ni taabu na ubatili, maana chapita upesi tukatokomea mara.”—Zaburi 90:10.
Yajapokuwa maendeleo ya kitiba, muda wa maisha ya mwanadamu bado ni sawa na vile ulivyokuwa katika siku ya Musa. Hata hivyo, binadamu hawatalaaniwa sikuzote kuwa na maisha yenye kupita haraka hivyo. Katika kitabu cha Biblia cha Isaya, Mungu alisema: “Kama siku za mti ndivyo zitakavyokuwa siku za watu wangu, na wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”—Isaya 65:22.
Mmoja wa miti yenye kuishi maisha marefu zaidi katika nchi za Biblia ni mzeituni. Mti unaoonyeshwa hapo juu ni mmoja wa mizeituni mingi wenye umri wa miaka elfu ambao bado unasitawi katika Galilaya. Ni lini binadamu watapata kuishi muda mrefu hivyo? Unabii huohuo waeleza kwamba itakuwa wakati Mungu atakapoumba “mbingu mpya na nchi mpya.”—Isaya 65:17.
Kitabu cha Ufunuo pia chatabiri kusimamishwa kwa “mbingu mpya na nchi mpya”—serikali mpya ya kimbingu na jamii mpya ya kibinadamu wakati Mungu “atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:1, 4.
Ahadi hii ya kimungu itatimizwa karibuni. Halafu, hata siku za mzeituni zitaonekana kama siku ya saa 24 tu. Na tutakuwa na wakati mwingi wa kuonea shangwe kwa ukamili kazi ya mikono yetu.