“Msiwe Wenye Kufungwa Nira Isiyosawazika”
FAHALI wawili wanaoonekana hapa wana nguvu nyingi ajabu, ikiwawezesha kuvuta mizigo mizito kwa urahisi. Lakini vipi kama fahali mmoja angeondolewa na mahali pake pawekwe punda. Kwa kuwa punda ni mdogo na mdhaifu kidogo kuliko fahali, yaelekea angeasi kwa kupiga teke mti unaomshika kwenye nira hiyo isiyosawazika. Basi, kukiwa na sababu nzuri, sheria ya Mungu kwa Israeli ilisema: “Usilime kwa ng’ombe na punda wakikokota jembe pamoja.”—Kumbukumbu la Torati 22:10.
Mtume Paulo aliandika jambo kama hilo kuhusu wanadamu. Alisema: “Msiwe wenye kufungwa nira isiyosawazika pamoja na wasio waamini.” (2 Wakorintho 6:14, NW) Jambo hilo hasa lapasa kukumbukwa tunapochagua mwenzi wa ndoa. Ndoa ni uhusiano wa kudumu, kwa kuwa Yesu Kristo alisema: “Aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.” (Mathayo 19:6) Uchungu mwingi wa moyo hutokea mume na mke wasipokuwa na itikadi moja, kanuni moja, na miradi sawa. Hivyo ni jambo la akili kufuata onyo hili la upole la Biblia la kuoa “katika Bwana tu.” (1 Wakorintho 7:39) Kuingia katika kifungo cha ndoa na mtu msiyeshiriki imani moja ya kidini laweza kutokeza tatizo kubwa zaidi hata kuliko kufunga kwa nira fahali pamoja na punda.
Tofauti ya itikadi ya kidini ni jambo moja tu liwezalo kufanya mume na mke wawe wamefungwa katika nira isiyosawazika. Watu wanaotazamia kuoana—hata wa dini moja—wangefanya vema kujiuliza, ‘Je, tuna miradi ileile? Tutaishi wapi? Nani atakayeshughulikia bajeti? Je, sote wawili tutafanya kazi? Vipi watoto? Je, fadhili na kufikiriana kutaongoza uhusiano wetu?’
Kwa kadiri fulani, njia ambayo masuala kama hayo yanazungumzwa yaweza kuonyesha kama nira itasawazika au haitasawazika. Bila shaka, hakuna watu wawili wanaofaana kabisa. Walakini, kwa ujumla ikiwa wanaotaka kuoana waweza kukabili matatizo na kuyatatua pamoja na ikiwa wanaweza kuwasiliana kwa ukawaida, yaelekea hawatafungwa nira isiyosawazika.