Utepe wa Kipaji cha Uso
Utepe unaovaliwa kwenye kipaji cha uso.
Ingawa Waisraeli waliambiwa kwamba walipaswa ‘kufunga sheria ya Mungu ikiwa ishara mkononi mwao’ na kuifanya iwe ‘utepe wa kipaji cha uso kati ya macho yao,’ kwa wazi jambo hilo halikurejezea kuvaa Maandiko kihalisi. (Kumbukumbu la Torati 6:6-8; 11:18, NW) Ni kweli kwamba waliagizwa wavae upindo halisi wenye matamvua kwenye mavazi yao ukiwa kikumbusho cha amri za Mungu. (Hesabu 15:38-40) Hata hivyo, uthibitisho wa kwamba “ishara” na ‘utepe wa kipaji cha uso’ zilikuwa ziwe za kitamathali waweza kuonwa katika maagizo ya Mungu kwa Waisraeli ya kuadhimisha jinsi alivyowaokoa. Mwadhimisho huo pia ulikuwa utumikie ‘ukiwa ishara mkononi mwako na ukiwa ukumbusho kati ya macho yako’ na ‘utepe wa kipaji cha uso kati ya macho yako.’—Kutoka 13:9, 14-16, NW.
Yaonekana Yehova alimaanisha kwamba Sheria ilipaswa kufuatwa kabisa kana kwamba wanaiona na kutimizwa kwa uangalifu kana kwamba iliandikwa katika bamba lililokuwa kati ya macho yao, na kana kwamba ilikuwa ishara mikononi mwao, ili kwamba, popote walipoangalia na chochote walichofanya, hawangekosa kuiona Sheria. Hata hivyo, muda fulani baada ya kurudi kutoka Babiloni, Wayahudi walianzisha dini ya kidesturi iliyotegemea mapokeo ya wanadamu, ambamo walitumia sheria hiyo kihalisi. (Mathayo 15:3, 9) Tepe za ngozi zilitumiwa na mafungu ya Maandiko kuandikwa kwazo, yaani Kutoka 13:1-10, 11-16; Kumbukumbu la Torati 6:4-9; 11:13-21. Angalau katika nyakati za baadaye, ngozi hiyo ilikunjwa na kuwekwa katika makasha madogo ya ngozi ya ndama na kufungwa kwenye kipaji cha uso na kwenye mkono wa kushoto. Wanaume Wayahudi walivaa hizo wakati wa sala za asubuhi, ila tu kwenye siku za msherehekeo na Sabato.
Yesu Kristo alishutumu unafiki wa waandishi na Mafarisayo ambao, kwa kutaka wengine waone uadilifu wao, walipanua makasha yao yenye kubeba maandiko waliyovaa yakiwa kama ulinzi. (Mathayo 23:2, 5) Neno la Kigiriki phy·la·kteʹri·on, “makasha ya ngozi,” ambayo ni makasha hayo yenye kubeba maandiko, hasa humaanisha askari-doria, nguzo, au ulinzi. Basi, hayo yalivaliwa yakiwa ulinzi, talasimu, au hirizi.
Hata hivyo, Biblia hushauri kwamba tusilinde sura nzuri au yenye uchaji Mungu bali tuulinde moyo. (Mathayo 23:27, 28; Mithali 4:23) Hiyo hukazia kwamba kile kitakachomfaidi mtu kabisa, si kuvaa Maandiko yaliyoandikwa kwenye mwili, bali ni kulinda hekima itumikayo na uwezo wa kufikiri na kupata uelewevu.—Mithali 3:21, 22; 4:7-9.