Acheni Nuru Yenu Ing’ae!
HATIMAYE wakati ulikuwa umewadia wa huyu mwanamume mzee kuona Mesiya aliyeahidiwa! Kwa ufunuo wa kimungu Simeoni alijua kwamba “hataona mauti kabla ya kumwona Kristo wa Bwana.” (Luka 2:26) Lakini ilisisimua kama nini wakati Simeoni alipoingia hekaluni na Mariamu na Yusufu kumweka mtoto Yesu mikononi mwake! Yeye alimsifu Mungu, akisema: “Sasa, Bwana, wamruhusu mtumishi wako, kwa amani . . . kwa kuwa macho yangu yameuona wokovu wako . . . nuru ya kuwa mwangaza wa Mataifa, na kuwa utukufu wa watu wako Israeli.”—Luka 2:27-32; linganisha Isaya 42:1-6.
Tangu ubatizo wake akiwa na umri wa miaka 30 hadi kifo chake, Yesu alithibitika kuwa “nuru” ya ulimwengu. Kwa njia zipi? Yeye alitoa nuru ya kiroho kwa kuhubiri juu ya Ufalme wa Mungu na makusudi Yake. Pia alifunua wazi mafundisho bandia ya kidini na kuonyesha waziwazi kazi za giza. (Mathayo 15:3-9; Wagalatia 5:19-21) Kwa hiyo, Yesu aliweza kusema kwa haki hivi: “Mimi ndimi nuru ya ulimwengu.”—Yohana 8:12.
Yesu alikufa mwaka wa 33 W.K. Je, nuru ilizimika wakati huo? Hata kidogo! Alipokuwa angali duniani, Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Nuru yenu na iangaze mbele ya watu.” (Mathayo 5:16) Vivyohivyo, baada ya kifo cha Yesu wafuasi wake waliendelea kudumisha nuru yao iking’aa.
Kwa kumwiga Yesu, Wakristo huonyesha nuru ya Yehova leo kwa kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Wao ‘huenenda kama watoto wa nuru,’ wakijithibitisha kuwa vielelezo vinavyong’aa katika maisha ya Kikristo.—Waefeso 5:8.