Wao Hupata Wapi Nguvu Zao?
UKITAZAMA kipepeo aliye kwenye picha hii, utaona kwamba mojawapo ya mabawa yake manne halitumiki kabisa. Hata hivyo, huyo kipepeo huendelea kula na kupepea. Hiki si kisa cha pekee. Vipepeo wameonekana wakifanya shughuli zao za kila siku bila asilimia 70 ya mabawa yao.
Vivyo hivyo, watu wengi huonyesha mwelekeo wenye nguvu. Licha ya kuteseka kutokana na matatizo ya kimwili au kihisia-moyo, hawakati tamaa.—Linganisha 2 Wakorintho 4:16.
Mtume Paulo mwenyewe alivumilia magumu mengi wakati wa zile safari zake za kimishonari. Alichapwa mijeledi, kupigwa, kupigwa kwa mawe, na kutiwa gerezani. Kwa kuongezea, alikuwa na aina fulani ya kutojiweza, labda tatizo la macho yake, ambalo lilikuwa “mwiba katika mwili” sikuzote.—2 Wakorintho 12:7-9; Wagalatia 4:15.
Mzee Mkristo aitwaye David aliyeshindana vikali na mishuko-moyo mibaya sana kwa miaka mingi, huamini kuwa msaada wa Yehova ulichangia sana kupona kwake. “Tena na tena, maendeleo yaliyopatikana kwa shida yalionekana kana kwamba yalikuwa yanapotea,” yeye aeleza. “Nilipokabiliwa na mvunjiko wa moyo kama huo, nilijiweka mikononi mwa Yehova, naye kwa kweli alinitegemeza. Kuna pindi ambazo nilisali kwa muda wa saa nyingi kwa wakati mmoja. Nilipozungumza na Yehova, hisia zangu za upweke na kutofaa kitu zilipotea. Nimeng’ang’ana kupitia pindi za udhaifu, na kwa sababu ya Yehova, udhaifu umetokeza nguvu—hata nguvu za kuwasaidia wengine.”
Yehova Mungu alimtia nguvu Paulo. Hivyo, aliweza kusema: “Niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu.” (2 Wakorintho 12:10) Ndiyo, udhaifu wa Paulo ulimfundisha kutegemea nguvu zitolewazo na Mungu. “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu,” akasema mtume. (Wafilipi 4:13) Kweli kweli Yehova huwapa nguvu watu wake.