Utimizo wa Unabii wa Biblia
KATIKA Imperial War Museum huko London, Uingereza, saa ya kipekee na kihesabu-tarakimu cha elektronia zimewekwa ili zionekane na watu. Hiyo saa inapozunguka, kihesabu-tarakimu hutoa mwaliko baada ya kila sekunde 3.31. Kwa kila mwaliko namba nyingine huongezwa kwenye jumla. Kila mwaliko, kila namba, huwakilisha, mwanamume, mwanamke, au mtoto ambaye amekufa kwa sababu ya vita katika karne hii.
Hicho kihesabu-tarakimu kilianza kurekodi kwacho mnamo Juni 1989 nacho chatazamiwa kumaliza huko kuhesabu usiku wa manane wa siku ya kuamkia mwaka wa 2000. Wakati huo tarakimu katika hicho kihesabu-tarakimu itafikia milioni mia moja—idadi inayokadiriwa ya vifo vinavyohusiana na vita katika karne yote ya 20.
Karibu miaka 2,000 iliyopita, Yesu Kristo alitabiri wakati ambao ungetiwa alama na ‘taifa kuondoka kupigana na taifa, na ufalme kupigana na ufalme.’ Kwa hiyo, Mashahidi wa Yehova wamekuwa wakihubiri kwa muda mrefu kwamba vita vyenye kufisha vya karne hii, pamoja na matetemeko mengi ya dunia, magonjwa ya kuambukiza, upungufu wa chakula, na mambo mengineyo, yote pamoja hutoa ithibati ya kwamba tunaishi katika “siku za mwisho”—kipindi cha wakati kinachofuatia kutawazwa kwa Kristo awe Mfalme mbinguni katika mwaka wa 1914.—Luka 21:10, 11; 2 Timotheo 3:1.
Likitumia Biblia kuwa mamlaka yalo, Mnara wa Mlinzi hutangaza habari njema ya kwamba karibuni Ufalme wa Mungu utaharibu waonezi na kugeuza dunia iwe paradiso. Na namna gani wakati ujao wa vita? Biblia hutaarifu hivi: “Njoni myatazame matendo ya BWANA, jinsi alivyofanya ukiwa katika nchi. Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari.”—Zaburi 46:8, 9.
[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 32]
Saa: Kwa Hisani ya Imperial War Museum