Faraja Wakati wa Miaka Minne ya Vita
WAKATI wa ile miaka minne ya vita katika eneo la iliyokuwa Yugoslavia, watu wengi walipatwa na magumu na upungufu mkali mbalimbali. Waliotiwa ndani yao walikuwa mamia ya Mashahidi wa Yehova, walioendelea kumtumikia “Mungu wa faraja yote” kwa uaminifu.—2 Wakorintho 1:3.
Katika Sarajevo, watu walipatwa na ule ugumu wa ziada wa kuishi katika jiji kubwa lililozingiwa wakati wote wa vita. Kulikuwa na upungufu wa nguvu za umeme, maji, kuni, na chakula. Kutaniko la Mashahidi wa Yehova la Sarajevo lilitendaje chini ya hali hizo zenye kupita kiasi? Wakristo kutoka nchi jirani walihatarisha uhai wao ili kuingiza kiasi kikubwa cha ugavi wa kitulizo. (Ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 1994, kurasa 23-27.) Pia, ndugu katika Sarajevo walishiriki mmoja na mwenzake, vitu walivyokuwa navyo, wakikazia zaidi kushiriki mambo ya kiroho. Wakati wa mazingiwa mwangalizi Mkristo kutoka jiji hilo alitoa ripoti ifuatayo:
“Twaithamini mikutano yetu sana. Mke wangu nami, pamoja na watu wengine 30, hutembea kilometa 15 [maili 9] kila safari kwenda mikutanoni. Wakati mwingine ilitangazwa kwamba maji yangetolewa wakati ambapo mikutano ilifanywa. Ndugu wangefanya nini? Je, wangekaa nyumbani au wangehudhuria mikutano? Ndugu zetu walipendelea kuihudhuria mikutano. Sikuzote ndugu husaidiana; chochote walicho nacho wao hushiriki mmoja na mwenzake. Dada mmoja kutanikoni mwetu huishi kwenye viunga vya hilo jiji, karibu na msitu; kwa hiyo ni rahisi zaidi kwake kupata kuni. Yeye pia hufanya kazi mahali pa kuokea mikate, na mshahara wake ni unga. Iwezekanapo, yeye huoka mkate mkubwa na kuuleta mkutanoni. Baada ya mkutano, aondokapo, yeye humpa kila mtu kipande.
“Ni jambo la maana kusiwe na ndugu na dada wowote wapatao kuhisi kuwa wameachwa peke yao. Hakuna ajuaye ni nani kati yetu atakayehitaji msaada wakati mwingine katika hali isiyopendeza. Tulipokuwa na barabara zenye barafu na dada mmoja alikuwa mgonjwa, ndugu wachanga, wenye nguvu, walimvuta hadi mikutanoni akiwa kwenye gari la kuteleza.
“Sisi sote hushiriki katika kazi ya kuhubiri, naye Yehova amebariki jitihada zetu. Ameona uhitaji wetu mkubwa katika Bosnia, lakini ametubariki kwa ongezeko—ongezeko ambalo hatukuwa tumeona kabla ya vita.”
Vivyo hivyo, katika sehemu nyingine zilizokumbwa na vita za iliyokuwa Yugoslavia, Mashahidi wa Yehova wamefurahia maongezeko licha ya magumu makali. Kutoka ofisi ya Kroatia ya Mashahidi wa Yehova yatoka ripoti hii juu ya kikundi cha Mashahidi: “Ndugu wanaoishi Velika Kladuša walikuwa na nyakati ngumu sana za kushughulika nazo. Mji huo ulishambuliwa kwenye pindi kadhaa. Ndugu walilazimika kueleza majeshi ya Kroatia, Serbia, na majeshi kadha wa kadha ya Kiislamu juu ya kutokuwamo kwao. Kwa hakika, walilazimika kuvumilia mengi—kufungwa gerezani, kuchapwa, njaa, hatari ya kifo. Na bado, wote walibaki wakiwa waaminifu na wana lile pendeleo lenye kutokeza la kuona baraka za Yehova juu ya utendaji wao mbalimbali.”
Yajapokuwa magumu hayo, Mashahidi wa Yehova katika Velika Kladuša na Bihać mji ulio jirani wanaendelea kufurahia maongezeko huku wakishiriki pamoja na jirani zao kwa bidii ujumbe wa Mungu wa faraja. Jumla ya watangazaji 26 wa Ufalme kutoka sehemu hizo mbili wanaongoza mafunzo ya Biblia ya nyumbani 39!