“Sisi Sote Ni wa Familia Ileile”
KATIKA miaka ya juzijuzi ubaguzi wa kidini na wa kijamii umeenea kotekote duniani. Tofauti za kikabila zimechochea mauaji, mateso, na ukatili mwingine mbalimbali wenye aibu. Kulingana na ripoti ya Amnesty International, ukiukaji mbalimbali wa haki za kibinadamu ulilazimisha watu zaidi ya milioni 23 ulimwenguni pote wakimbie makao yao katika 1994.
Katika Rwanda peke yayo, karibu watu 500,000 walichinjwa na wengine zaidi ya 2,000,000 wakawa wakimbizi baada ya jeuri kutokea kati ya Watutsi na Wahutu. “Mashahidi wa Yehova hasa walinyanyaswa,” laripoti gazeti la habari la Ubelgiji Le Soir, “kwa sababu ya kukataa kwao kuchukua silaha.” Mashahidi wa Yehova hawashiriki katika mapambano ya silaha. Hata hivyo, mamia yao yaliuawa katika jeuri hiyo. Hilo latukumbusha maneno ya Yesu kwa wanafunzi wake: “Kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, . . . ulimwengu huwachukia.”—Yohana 15:19.
Familia moja ya Mashahidi—Eugène Ntabana, mke wake, na watoto wake wawili—iliishi katika jiji kuu, Kigali. Alipokuwa akiwaeleza majirani wake juu ya kutokuwamo kwa Kikristo, mara nyingi Eugène alisema juu ya mmea bougainvillea, mmea upandao unaositawi katika tabia za nchi zenye joto.—Mathayo 22:21.
“Huku Kigali,” Eugène alikuwa akieleza, “mmea bougainvillea hutokeza maua mekundu, mekundu-meupe, na nyakati nyingine meupe. Hata hivyo, yote hayo ni ya familia ileile. Ndivyo ilivyo na wanadamu. Ingawa huenda tukawa wa jamii, rangi ya ngozi, au malezi tofauti ya kikabila, sisi sote ni wa familia ileile, familia ya wanadamu.”
Kwa huzuni, ijapokuwa hali yao yenye amani na msimamo wao wa kutokuwamo, familia ya Ntabana iliuawa kimakusudi na kikundi cha wafanya-ghasia chenye tamaa ya kumwaga damu. Hata hivyo, walikufa wakiwa waaminifu. Twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova Mungu atatimiza ahadi yake kwa watu wa jinsi hiyo, nao watafufuliwa ili kuurithi ulimwengu ambamo ubaguzi hautakuwako tena. (Matendo 24:15) Ndipo, familia ya Ntabana, pamoja na nyinginezo, ‘zitajifurahisha kwa wingi wa amani.’—Zaburi 37:11.