‘Wao Wanapendezwa na Kuwasaidia Wengine’
HILO ndilo alilosema polisi wa New York City kuhusu Mashahidi wa Yehova. Alikuwa akisema na Kathleen, mmojawapo wajitoleaji wa wakati wote anayetumikia kwenye makao makuu ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York.
Wakati wake wa kupumzika mchana, siku ya vuli yenye joto na jua, Kathleen aliketi kwenye benchi kwenye kijia kiitwacho Promenade kilicho karibu. Alikuwa akisikiliza chombo cha kuchezea kaseti chenye hedifoni. Kwenye kituo cha helikopta ng’ambo ya Mto East, matayarisho ya kuondoka kwa papa aliyekuwa amekuwa akizuru hilo jiji, yalikuwa yakiendelea. Ulinzi ulikuwa mkali kila mahali, na polisi kadhaa walikuwa wakishika doria kwenye Promenade. Mmoja wao akamfikia Kathleen na kumuuliza alilokuwa akifanya. Kathleen akajibu hivi: “Nasikiliza tepu ya lugha ya Kirusi. Waona, mimi ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova, nami nataka kujifunza Kirusi ili nishiriki habari njema ya Ufalme wa Mungu pamoja na watu wenye kusema Kirusi ambao wamekuja kuishi jijini.”
Polisi huyo akaitikia kwamba alikuwa amekuja kuwapenda Mashahidi wa Yehova hatua kwa hatua katika miaka yake 15 iliyopita akiwa ofisa doria katika New York City. Alisema hivi: “Nawaona Mashahidi wa Yehova kuwa dini iliyopangwa kitengenezo ambayo washiriki wayo wanapendezwa kwa moyo mweupe na kuwasaidia wengine katika jumuiya.”
Mashahidi wa Yehova wanajulikana ulimwenguni pote kwa kazi wanayofanya ya kuhubiri mlango hadi mlango. (Matendo 20:20) Ingawa wanaelekeza kwenye Ufalme wa Mungu kuwa suluhisho pekee kwa matatizo yanayowakumba watu, wao husaidia watu pia waboreshe hali yao ya maisha kwa kuwatia moyo watumie kanuni za Biblia katika maisha yao ya kila siku. Kwa kielelezo, Mashahidi husihi sana wazazi waandae mazingira yanayofaa masomo nyumbani. Wao wanawahimiza watu mmoja-mmoja wawe wenye kufuatia haki na wenye kutii sheria, wakiwatia moyo wapate stadi na sifa ambazo mwajiri ataona kuwa zenye thamani.
Ndiyo, Mashahidi wa Yehova wanapendezwa sana na kuwasaidia watu katika jumuiya waboreshe maisha zao. Wakaribishwa kwa uchangamfu uitikie mwito ufuatao.