Ni Nani Watakaokuwa Waeneza-Evanjeli?
KWENYE mkutano wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni miaka 40 hivi iliyopita, washiriki walisihiwa sana “watokeze roho ya kueneza evanjeli” na wafundishe makundi yao “yaende yakieneza evanjeli.” Miaka mitano baadaye John A. O’Brien, kasisi Mkatoliki, aliandika juu ya uhitaji wa kuwaleta wanafunzi wapya “kwa kuwaendea” wala si kwa “kuketi tu nyumbani mwetu.” Na katika Januari 1994, Papa John Paul II alisema kwamba “huu si wakati wa kuiaibikia Gospeli, ni wakati wa kuihubiri kutoka juu ya paa za nyumba.”
Yaelekea miito hiyo ya pindi kwa pindi ya kupata waeneza-evanjeli imeangukia masikio yasiyosikia. Makala kwenye gazeti la habari la Australia Illawarra Mercury ilitaarifu hivi: “Wakatoliki wa Mwambao wa Kusini wajulikanao sana hawana hamu ya kukubali kirasmi na kutumia katika imani yao njia ifuatwayo na Mashahidi wa Yehova.” Mtu mmoja alisema kwamba kueneza evanjeli “si sehemu [kwa vyovyote] ya mwelekeo wa akilini wa Ukatoliki.” Mwingine alisababu hivi: “Ni vema Kanisa lijiendeleze, lakini si kupitia kubisha milango. Labda kupitia shule au kutuma barua kungekuwa bora.” Hata mkuu wa makasisi wa kathedro ya huko hakuwa na hakika sana juu ya jinsi ya kufasiri maelezo ya papa. “Tungewatia watu moyo wazoee Gospeli waijuayo katika maisha yao wenyewe,” akasema. “Iwe hilo lamaanisha kubisha milango ni jambo jingine.” Kichwa kikuu cha makala ya habari chatoa muhtasari vizuri: “Wakatoliki hawatatii mwito wa Papa wa kuhubiri.”
Licha ya kushindwa kueneza evanjeli kwa Jumuiya ya Wakristo, Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni tano wanafuata amri ya Yesu ya ‘kufanya mataifa yote kuwa wanafunzi.’ (Mathayo 28:19, 20; linganisha Matendo 5:42.) Kuhubiri kwao mlango hadi mlango sasa kwafanywa katika nchi zaidi ya 230. Ujumbe waletao ni wenye kufaa, ukionyesha waziwazi ahadi za ajabu za Biblia za wakati ujao. Kwa nini usizungumze nao wakati ujao wakutembeleapo?