Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w96 12/15 kur. 20-21
  • “Basi Kanisa Lenu Liko Wapi?”

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Basi Kanisa Lenu Liko Wapi?”
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
w96 12/15 kur. 20-21

“Basi Kanisa Lenu Liko Wapi?”

MASHAHIDI WA YEHOVA katika Msumbiji huulizwa swali hilo mara nyingi. Kwa kweli, kufikia majuzi limekuwa swali gumu la kujibu. Limekuwa hivyo kwa sababu Mashahidi wa Yehova hawakuwa na utambuzi wa kisheria katika nchi hiyo mpaka 1991. Kwa sababu hiyo, haikuwezekana kuwa na mahali pa ibada palipotambulika waziwazi na palipo mathubuti.

Hata hivyo, hali hiyo ilibadilika Februari 19, 1994. Siku hiyo yenye joto na jua kali, Majumba ya Ufalme mawili ya kwanza yaliyopata kujengwa Msumbiji yaliwekwa wakfu. Jumla ya watu 602 walikuja kwenye kuwekwa wakfu kwa mahali hapo pazuri pa kukutania katika jiji la bandari la Beira, karibu katikati ya pwani ya Msumbiji. Yatashughulikia mahitaji ya makutaniko matatu katika jiji hilo.

Mradi wote, tangu kuweka msingi hadi kumaliza majengo, ulichukua mwaka mzima na miezi miwili ya kazi ngumu. Mara nyingi wajitoleaji 30 au zaidi kutoka Zimbabwe iliyo jirani walikuja kufanya kazi bega kwa bega pamoja na Mashahidi wa Msumbiji. Kwa kuwa si wote walioweza kuishi katika makao ya mishonari katika Beira, ambayo yalitumika yakiwa kitovu cha utendaji, baadhi yao walipiga kambi nje kuyazunguka hayo makao wakati wa miisho-juma na kwenye pindi fulani kwa majuma kadhaa mfululizo.

Mahali pa ujenzi pa Jumba la Ufalme la Makutaniko ya Massamba na Munhava pako kwenye barabara kuu ya Beira. “Siku yenye shughuli nyingi, wakati ambapo kazi iliendelea haraka na maendeleo yalionekana sana,” akaonelea mishonari mmoja, “tuliona zilizokaribia kuwa aksidenti huku madereva walipokuwa wakipitia hapo walipokodolea macho hilo Jumba la Ufalme, karibu wakisahau sukani zao.” Wengi walisimama watazame kazi, nao walivutiwa hasa na kuwapo kwa jamii mbalimbali za watu wakifanya kazi pamoja kwa umoja.

Matayarisho na kupanga kwingi kulihusishwa katika hiyo kazi. Tofauti na miradi mingine mingi katika sehemu hii ya ulimwengu, ambako maunzi na mali ni adimu, kazi katika Majumba ya Ufalme hayo haikutua kamwe kwa sababu ya ukosefu wa ugavi. Kwenye pindi moja, mifuko 800 ya sementi ilihitajiwa, na mahali pekee ambapo ingeweza kupatikana hapakuwa na mifuko iliyohitajiwa ya kubebea sementi. Ndugu waliwasiliana na ofisi ya tawi ya Watch Tower Society katika jiji kuu, Maputo; mifuko ilitumwa kwa ndege, ikapelekwa kwenye kiwanda cha sementi, na kujazwa. Kazi iliendelea bila kukatizwa.

Kwenye pindi nyingine, wakati ambapo mikingiko ya paa ilipokuwa ikiwekwa, hicho kikundi cha wafanyakazi kilipungukiwa na mihimili ya feleji. Kwa sababu ya uadimu mkubwa, feleji ya mradi huo ilikuwa imeingizwa nchini kutoka umbali wa kilometa 600! Mtu aliyekuwa akitazama alifikiwa na mfanyakazi mmoja wa kile kikundi cha wafanyakazi na kuulizwa ikiwa alijua mahali ambapo wangeweza kupata feleji za kumaliza ile kazi. Mtu huyo alijibu hivi: “Nimekuwa nikisimama hapa kwa muda wa zaidi ya saa nzima, na haikuwa kwa sadfa. Siwezi kujizuia nisipendezwe na kazi mnayofanya na roho ya mradi huu. Mimi nina aina ya feleji mnayohitaji, na ningependa kuwapa ikiwa zawadi.” Hilo likawa uandalizi wa wakati ufaao.

Watazamaji wengi walitaka kujua ni shirika gani kubwa la ujenzi lililosimamia huo mradi. Hicho kikundi cha wafanyakazi bila shaka kilifurahia kuwaambia kwamba hao walikuwa Mashahidi wa Yehova waliokuwa wakitoa kwa hiari huduma zao mbalimbali. Ni nini hasa kilichowavutia watazamaji? “Ninyi ni watu wenye muungano,” akasema mmoja. “Ingawa ninyi ni wa jamii tofauti-tofauti, mwafanya kazi pamoja kama ndugu.” Tokeo lilikuwa kwamba wengi walikuja kuomba mafunzo ya Biblia. Hilo limeathiri pia mikutano. Kwa kielelezo, wastani wa hudhurio la mikutano la Kutaniko la Manga, ni zaidi ya maradufu ya idadi ya Mashahidi.

Kwa kweli hayo Majumba ya Ufalme mapya yamethibitika kuwa baraka kubwa kwa Mashahidi wa mahali hapo. Walio wengi walikuwa wamekutanika hapo mbele katika mahali pa kikale penye paa la nyasi au mabati machache yaliyokuwa paa, katika uwanja wa nyuma ya nyumba, au katika chumba kidogo cha nyumba ya faragha. Mara nyingi waliloa kuliponyesha; bado walihudhuria mikutano kiaminifu. Kwa miongo kadhaa hayo yalikuwa ndiyo “Majumba ya Ufalme” pekee waliyojua Mashahidi katika Msumbiji. Ndugu Caetano Gabriel, mzee katika Kutaniko la Massamba, alitangaza hivi: “Twawashukuru ndugu zetu ulimwenguni pote ambao walichangia kufanikiwa kwa mradi huu.” Shahidi kijana mmoja alikumbuka hivi: “Tulipokuwa Carico (“kambi za kuelimishwa upya” ambamo Mashahidi wa Yehova walifungiwa kwa yapata miaka 12), tulizoea kusema, ‘Tutavulimia kiaminifu, na Yehova atatuthawabisha.’ Jumba la Ufalme jipya ni thawabu kutoka kwa Yehova.” Maneno yao yaonyesha shukrani zao zenye kina na azimio lao la kumsifu Yehova.

Vijana wengi walioshiriki katika kazi ya ujenzi walitiwa roho ya upainia na baadaye walichukua huduma ya upainia wa kawaida. Kijana Isabel, painia wa kawaida katika Kutaniko la Manga, alitoa elezo hili baada ya kuona Jumba la Ufalme lililotakata kwa usafi siku moja kabla ya kuwekwa wakfu kwalo: “Kwangu mimi hapa ndipo mahali pazuri zaidi katika jiji la Beira. Ni furaha kubwa zaidi kwangu kuwa hapa.” Mishonari, Adão Costa, alieleza kwamba wenye mamlaka wa huko walishirikiana sana katika kuruhusu taratibu za pekee za kuingiza vitu kutoka nchi nyingine kwa sababu walijua juu ya ufuatiaji wa haki wa Mashahidi. Kisha akaongeza hivi: “Ingawa tulichoka sana, tulikuwa na furaha kuona matunda ya kazi hiyo yote kwa heshima na utukufu wa Yehova.”

Sasa, wakati wowote ambapo mkazi mwenye urafiki wa jiji la Beira aulizapo, “Basi kanisa lenu liko wapi?” hao Mashahidi humwelekeza kwenye mojawapo Majumba ya Ufalme mapya mawili na kuitikia kwa maneno kama, “Liko kwenye International Road, Avenida Acordo de Lusaka, ng’ambo ya Fourth Squadron Police Station.” Kisha, waongeza sahihisho moja wakisema hivi, “Ila si kanisa. Ni Jumba la Ufalme!”

[Picha katika ukurasa wa 20]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

AFRIKA

MSUMBIJI

Beira

Maputo

[Hisani]

Ramani: Mountain High Maps® Copyright © 1995 Digital Wisdom, Inc.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki