Ni Nani Anayeongoza Mambo?
“NI NANI anayeutawala ulimwengu?” Ikiwa mtu fulani angekuuliza swali hilo, ungejibuje? Watu wa kidini walio wengi huenda wakasema “Mungu” au “Yesu.” Makala katika gazeti la habari la Bahamas, The Freeport News, lilitoa jibu ambalo wachache wangetazamia.
“Nilipata trakti mlangoni kwangu,” ndivyo aanza mwandishi wa hiyo makala. “Kwa kawaida huwa sisomi habari ya jinsi hiyo, lakini wakati huo nikaamua kuisoma. Kichwa kiliuliza, ‘Ni Nani Hasa Anayeutawala Ulimwengu?’” Kwa kuisoma trakti hiyo yenye msingi wa Biblia, mwanamke huyo alijifunza kwamba mtawala wa ulimwengu huu si Mungu wala si Yesu bali ni Shetani Ibilisi.—Yohana 12:31; 14:30; 16:11; 1 Yohana 5:19.
“Fikiria ukatili wa kinyama wa umwagaji damu mwingi usio na huruma,” trakti hiyo ikafafanua. “Wanadamu wametumia vyumba vya gesi, kambi za mateso, silaha zenye kutupa moto, mabomu ya petroli inayowaka moto, na njia nyinginezo zinazochukiza ili kutesana na kuchinjana bila huruma. . . . Ni kani gani zinazowasukuma watu kutenda maovu yenye kuchukiza au kuwaongoza katika hali ambazo wanahisi ni lazima wafanye mambo ya ukatili? Je! umepata kujiuliza ikiwa uwezo fulani mwovu usioonekana unawaongoza watu kufanya matendo hayo ya jeuri?” Je, ni jambo la kushangaza kwamba Biblia humwita Shetani “mungu wa huu mfumo wa mambo”?—2 Wakorintho 4:4.
Kwa furaha, wakati uko karibu ambapo Shetani na roho waovu wake hawatakuwako tena. “Ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.” (1 Yohana 2:17) Ndiyo, Biblia huahidi kwamba wale wafanyao mapenzi ya Mungu ndio watakaokuwa na tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. (Zaburi 37:9-11; 2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Kuondolewa kwa uvutano mwovu wa Shetani na roho waovu wake kutakuwa kitulizo kama nini!
Baada ya kutoa muhtasari wa yaliyomo katika trakti hiyo ndogo, mwandishi wa makala ya The Freeport News alifikia mkataa huu: “Naterema kwa kweli kwamba nilisoma trakti hiyo . . . kwa sababu mimi pia nimehangaikia hali ya ulimwengu, na ni nani anayeongoza mambo.”