Kukinza Mashtaka Yasiyo ya Kweli Katika Ufaransa
MAJUZI Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa walielekezewa mfululizo wa mashtaka yasiyo ya kweli. Vikitumia kwa faida yavyo matukio yenye kuhuzunisha yaliyohusisha madhehebu ya kidini katika Ulaya na Japani, vyombo vya habari vilieneza habari iliyopotolewa juu ya Mashahidi. Walifananishwa kimakosa kuwa mojawapo ya madhehebu yaliyo makubwa zaidi na yaliyo hatari zaidi.
Wakijitahidi kurekebisha mambo, Mashahidi wa Yehova walichapisha trakti iliyojibu maswali kama vile: Mashahidi wa Yehova ni nani? Je, wao ni Wakristo? Je, wanakubali utunzaji wa kitiba? Kwa nini wanaenda kutoka mlango hadi mlango? Kazi yao inagharimikiwaje? Mashahidi wa Yehova wanaifaidije jumuiya?
Trakti hiyo ya lugha ya Kifaransa yenye kuarifu ilikuwa na kichwa Jehovah’s Witnesses—What You Need to Know (Mashahidi wa Yehova—Unayopaswa Kujua). Ili kuwaachia watu wengi iwezekanavyo trakti hiyo, kampeni ilipangwa. Kuanzia Mei 13 hadi Juni 9, 1996, nakala zaidi ya milioni tisa ziligawanywa.
Trakti hiyo iliwapendeza wengi, kutia na maofisa wa umma. “Uchambuzi ulioelekezewa Mashahidi wa Yehova wanighadhibisha,” akaandika diwani wa kimkoa baada ya kuisoma hiyo trakti. “Mara nyingi nimekuja kuthamini kazi yenu ya ukarimu na isiyo na ubinafsi.” Akiitikia trakti hiyo, mshiriki wa Bunge la Ulaya aliandika hivi: “Watu walio wengi wanajua vema jinsi ya kutofautisha kati ya kikundi cha Wakristo mlicho nyinyi na yale madhehebu.”
Katika Brittany Shahidi mmoja alimtolea kasisi hiyo trakti, ambaye aliikubali kwa utayari. “Nawapongeza kwa yale mnayofanya,” akasema kasisi huyo. Kisha akaongeza hivi: “Nawatia moyo wanaparokia wangu wawakaribishe nyumbani mwao na kuwapa kikombe cha kahawa. Hata mwaweza kuwaambia wale mnaokutana nao kwamba mmekuwa nyumbani mwangu. Pia nataka kuwaambia kwamba nathamini kusoma vichapo vyenu.”
Baada ya kupokea hiyo trakti, mwanamume Mprotestanti katika Alsace aliandikia Watch Tower Society akiomba funzo la Biblia. “Nikiwa nimepoteza uhakika wote katika parokia yangu,” akaandika, “natazamia mwanzo mpya wa kiroho.” Yajapokuwa mashtaka yasiyo ya kweli ambayo mara kwa mara huelekezwa kwao, Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa—kwelikweli, katika sehemu zote za ulimwengu—wanaendelea kuwasaidia watu wapate ujuzi sahihi juu ya makusudi ya Mungu, kama yalivyo katika Biblia.—2 Timotheo 3:16, 17.