Kuchukua Nira Wakati wa Ujana
KATIKA hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” vijana hukabili misongo mingi. (2 Timotheo 3:1) Wao hushambuliwa kila siku na propaganda zichocheazo ukosefu wa adili, kuvuta sigareti, na namna nyinginezo za tabia yenye kuharibu. Huenda wale wanaofuata viwango vya Biblia wakadhihakiwa kwa kutokubaliana na umati, na huenda Wakristo fulani wakahisi kwamba ingekuwa rahisi zaidi kusalimu amri.
Kuelekea mwisho wa karne ya saba K.W.K., Yeremia aliandika hivi: “Ni vema mwanadamu aichukue nira wakati wa ujana wake.” (Maombolezo 3:27) Alimaanisha nini? Kwamba kujifunza kukabiliana na majaribu wakati wa ujana husaidia kutayarisha mtu kukabili magumu ya utu uzima. Ijapokuwa majanga hayapendezi, hayaepukiki kwa Wakristo vijana na watu wazima. (2 Timotheo 3:12) Lakini manufaa za uaminifu ni nyingi kuliko kitulizo chochote cha kipindi fulani ambacho kuridhiana huenda kukaleta.
Ikiwa wewe ni kijana, kabili majaribu ya imani kikamili. Ushawishiwapo kushiriki katika mwenendo mbaya, kataa kuridhiana. Ijapokuwa huenda kwa wakati huu ikawa vigumu kufanya hivyo, utakuwa na mahangaiko machache maishani mwako. Yesu aliahidi hivi: “Chukueni nira yangu . . . , nanyi mtapata burudisho kwa ajili ya nafsi zenu. Kwa maana nira yangu ni ya fadhili na mzigo wangu ni mwepesi.”—Mathayo 11:29, 30.
Kubali mwito wa kuishi kulingana na viwango vya Biblia. Kufanya hivyo kutakupatia njia iliyo bora zaidi ya maisha sasa na tumaini hakika la wakati ujao. Kama vile Biblia hutaarifu, “ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.”—1 Yohana 2:17.