‘Nitamkimbilia Mungu’
KATIKA “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” vishawishi na misongo zaongezeka daima. Kwa kielelezo, ufuatiaji wetu wa haki huenda ukatahiniwa kazini. Usafi wetu wa kiadili huenda ukatahiniwa miongoni mwa wanashule wenzetu. Na uaminifu-maadili wetu hutahiniwa mara nyingi na ulimwengu ulio mfisadi kiadili.—2 Timotheo 3:1-5.
Mwandikaji wa Biblia Asafu pia aliishi wakati ambapo uovu ulisitawi. Baadhi ya watu walioishi wakati uleule wake hata walijivunia mwenendo wao usio wa kumwogopa Mungu. “Kiburi kimekuwa mkufu shingoni mwao,” akaandika Asafu. “Jeuri huwavika kama nguo. Hudhihaki, husimulia mabaya, husimulia udhalimu kana kwamba wako juu.” (Zaburi 73:6, 8) Je, waujua mtazamo huo?
Kwa wale wanaotamani kufanya yaliyo sawa, mwenendo huo wasononesha sana, hata wavunja moyo. “Mchana kutwa nimepigwa,” akaomboleza Asafu. “Ikawa taabu machoni pangu.” (Zaburi 73:14, 16) Huenda ukahisi vivyo hivyo, lakini usikate tumaini! Asafu aliweza kukabiliana na uovu wa siku yake, nawe hali kadhalika waweza kufanya hivyo. Lakini jinsi gani?
Asafu alikuja kung’amua kwamba ni vigumu kupata haki ya kweli chini ya utawala wa mwanadamu usio mkamilifu. (Zaburi 146:3, 4; Mithali 17:23) Hivyo badala ya kupoteza wakati, nishati, na mali zake zenye thamani akijaribu kuondolea mbali uovu wote uliomzunguka, alikazia fikira uhusiano wake na Mungu. Asafu alitangaza hivi: “Kumkaribia Mungu ni kwema kwangu; nimefanya kimbilio kwa Bwana MUNGU.”—Zaburi 73:28.
Leo, wale wanaoshiriki katika mazoea ya biashara yenye ufisadi mara nyingi hupata faida za kimwili. Hata huenda wengi wakajivunia kupuuza kwao sheria za kiadili za Mungu. Lakini hawatashinda kwa wakati usio dhahiri. “Hakika Wewe huwaweka penye utelezi,” akaonelea Asafu. “Huwaangusha mpaka palipoharibika.”—Zaburi 73:18.
Ndiyo, kwa wakati wa Mungu ufaao, ujanja, ujeuri, na ufisadi, na pia mazoea mengine yoyote ya kutomwogopa Mungu ambayo Wakristo wa kweli wanalazimika kuepuka, yataondolewa mbali. Biblia yaahidi hivi: “Watenda mabaya wataharibiwa, bali wamngojao BWANA ndio watakaoirithi nchi.” (Zaburi 37:9) Kwa sasa, na tuige maneno ya mtunga-zaburi aliyesema hivi: “BWANA ni jabali langu, na boma langu, na mwokozi wangu, Mungu wangu, mwamba wangu ninayemkimbilia.”—Zaburi 18:2.