Taa ya Kukuongoza Kwenye Kijia cha Maisha
“EE BWANA, najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Kwa maneno hayo nabii Yeremia alionyesha kwamba wanadamu hawawezi kutembea katika kijia cha maisha bila msaada. Msaada huo waweza kupatikana wapi? Mtunga-zaburi ajibu katika sala yake kwa Yehova Mungu: “Neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu.”—Zaburi 119:105.
Wanaojifunza Neno la Mungu, Biblia Takatifu, na kutumia isemayo watakuwa sawa na mtu aanzaye safari asubuhi na mapema. Mwanzoni, hawezi kuona mengi kwa sababu kuna giza. Lakini jua lianzapo kuchomoza, aona zaidi na zaidi. Hatimaye, jua laangaza moja kwa moja juu ya kichwa chake. Aona kila kitu kwa udhahiri kabisa. Kielezi hicho chakumbusha mithali moja ya Biblia: “Njia ya wenye haki ni kama nuru ing’aayo, ikizidi kung’aa hata mchana mkamilifu.”—Mithali 4:18.
Namna gani wanaokataa mwongozo wa Mungu? Biblia husema hivi: “Njia ya waovu ni kama giza; hawajui ni kitu gani kiwakwazacho.” (Mithali 4:19) Ndiyo, waovu ni kama mtu ajikwaaye gizani. Hata yaonekanayo kuwa mafanikio yao ni ya muda tu hata chini ya hali zenye kufaa zaidi, kwa kuwa “hapana hekima, wala ufahamu, wala shauri, juu ya BWANA.”—Mithali 21:30.
Kwa hiyo, fuata mwongozo wa Neno la Mungu, Biblia. Ukifanya hivyo, utakuta kwamba maneno haya ya Mithali 3:5, 6 ni ya kweli: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.”