Je, Mungu Atauangamiza Ulimwengu?
KULINGANA na Papa John Paul wa Pili, wanadamu waweza kutazamia kwa hamu wakati ujao wakiwa na uhakika. Katika historia yote, alisema, “watu wameendelea kufanya dhambi, labda kubwa zaidi kuliko zile zilizofafanuliwa kabla ya furiko,” akasema. Ijapokuwa hivyo, papa alieleza, “kutokana na maneno ya agano la Mungu alilofanya na Noa twang’amua kwamba sasa hakuna dhambi iwezayo kumfanya Mungu auangamize ulimwengu ambao yeye mwenyewe aliumba.”
Je, ni kweli kwamba Mungu hatauangamiza ulimwengu kamwe? Biblia hutaarifu kwamba baada ya Gharika, Mungu alimwambia Noa hivi: “Wala kila chenye mwili hakitafutwa tena kwa maji ya gharika; wala hakutakuwa tena gharika, baada ya hayo, kuiharibu [“kuiangamiza,” NW] nchi.” (Mwanzo 9:11) Papa asema kwamba kwa maneno hayo, Mungu “alijiweka mwenyewe chini ya wajibu wa kuhifadhi [dunia] asiiangamize.”
Biblia hufanya ieleweke wazi kwamba Muumba hataruhusu sayari yetu iangamizwe. “Dunia hudumu daima,” yasema Biblia. (Mhubiri 1:4) Lakini kuna mengi zaidi ya kujifunza kutokana na Gharika—jambo fulani ambalo papa hakueleza.
Yesu alisema kwamba hali duniani wakati wa kuwapo kwake kwa wakati ujao zingekuwa “kama vile siku za Noa zilivyokuwa,” wakati ambapo watu “hawakujali mpaka furiko likaja na kuwafagilia mbali wote.” (Mathayo 24:37-39) Vivyo hivyo, mtume Petro aliandika kwamba kama vile “ulimwengu wa wakati huo uli[vyo]patwa na uangamizo ulipogharikishwa kwa maji,” ndivyo pia “siku ya hukumu na ya uangamizo wa watu wasiomwogopa Mungu” yatisha ulimwengu wa sasa.—2 Petro 3:5-7.
Je, Yesu na Petro walisahau agano la Mungu pamoja na Noa? La hasha! Kama vile alivyotaarifu katika agano pamoja na Noa, Mungu hatatumia maji ya mafuriko kumaliza mfumo huu mwovu wa mambo. Badala yake, atatumia nguvu za “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,” Yesu Kristo. (Ufunuo [Apokalipsi] 19:11-21) Kwa hiyo, kulingana na Biblia, dunia haitaangamizwa, lakini “ulimwengu” wa wanadamu waovu bila shaka utafikia mwisho. (Mithali 2:21, 22; Ufunuo 11:18) Baadaye, “wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:29.