“Nyinyi Mko Vile Ambavyo Mungu Hututazamia Tuwe”
WAKISHIRIKIANA na mamlaka za kilimwengu “kwa ajili ya Bwana,” Wakristo wanaweza kutazamia kupokea “[sifa wakiwa] watenda-mema.” (1 Petro 2:13-15) Mashahidi wa Yehova katika Afrika Kusini walijionea jambo hilo muda mfupi uliopita, kwenye mkusanyiko wa wilaya walioufanya katika jumba la chuo fulani.
Siku ya kwanza ya mkusanyiko huo, polisi wa usalama wa chuo hicho walijiandaa kukabili idadi ya kawaida ya wajumbe wenye hasira na wasioshirikiana, kama walivyopata kuona katika mikusanyiko ya namna nyingine. Hata hivyo, kwa kuwa hawakupata kamwe kuwa na shughuli pamoja na Mashahidi wa Yehova, kwa hakika walikuwa waone jambo ambalo hawakutazamia!
Ikiwa sehemu ya ukaguzi wa kawaida kwenye malango, polisi wa usalama walipekua kila gari lililokuwa likiingia na kuondoka mahali hapo. Walistaajabu waliposalimiwa kwa urafiki, subira, na staha, hata ingawa upekuzi huo uliwachelewesha wajumbe hao. Hakukuwa na ukinzani wowote ambao kwa kawaida unakuwepo, wala kubishana, wala usemi wenye kuudhi. “Tofauti na wageni wale wengine,” akasema afisa mmoja wa usalama, “mwaonyesha roho ya unyenyekevu na adhama tulivu iliyo wazi kwetu sote.”
Mkuu wa usalama alipojua juu ya mwenendo wenye kushirikiana wa Mashahidi wa Yehova, aliamua kwamba haikuwa lazima kupekua magari yao “kwa sababu,” yeye akasema, “nyinyi mmefundishwa nidhamu ifaavyo.” Kwa sababu hiyo, magari yaliyotambuliwa kwa vibandiko vya upakizi vyenye herufi “MY” yaliruhusiwa kuingia bila kupekuliwa.
Mwishoni mwa mkusanyiko, mkuu wa ulinzi alisema kwamba alitumaini kuwaona Mashahidi tena karibuni. “Hatujapata kamwe kuona watu wenye tabia nzuri hivyo,” akasema. “Nyinyi mko vile ambavyo Mungu hututazamia tuwe.” Pongezi hiyo ni kichocheo cha ziada kwa Wakristo wa kweli ‘kudumisha mwenendo bora,’ ili watu ‘wamtukuze Mungu kwa sababu ya kazi bora ambazo wamekuwa mashahidi wa kujionea.’—1 Petro 2:12.