“Mzoeze Mtoto”
ILI ukulima uwe wenye mafanikio, mtu ahitajiwa kufanya mengi zaidi ya kutawanya mbegu ardhini kisha kurudi kuvuna baada ya miezi kadhaa. Kazi nyingi iliyo ngumu inahusika katika kutayarisha udongo, kupanda mbegu, kisha kutia maji na kurutubisha mimea ili iweze kukua kufikia ukomavu.
Kazi hiyo yaweza kuonyesha vizuri ukweli wa andiko la Mithali 22:6, lisemalo hivi: “Mlee [“mzoeze,” NW] mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” Kwa kweli, mazoezi ya wazazi huchangia sana katika kulea mtoto kwa mafanikio.
Hata hivyo, katika ulimwengu wa leo wenye uendekevu, wazazi wengi hushindwa kusikiza shauri hilo. Wanapofuata hekima ya kawaida kwamba watoto lazima wajifunze kushughulikia matatizo peke yao, mara nyingi watoto wao huachwa wajitegemee. Kufanya hivyo huwaacha wachanga wakiwa wanaweza kudhuriwa na uvutano wenye madhara wa watu wapotovu, wasio na maadili.—Mithali 13:20.
Ni jambo bora kama nini kwa wazazi kuwafundisha watoto wao kanuni za Kikristo hatua kwa hatua kupitia mazoezi ya kimungu wanapokuwa na umri mdogo! Umri mdogo kadiri gani? “Tangu utoto sana,” asema mtume Paulo. Ilikuwa hivyo kwa mwanamume mchanga, Timotheo. Mama yake, Eunike, na nyanya yake Loisi walikaza kikiki “maandishi matakatifu” kwa Timotheo hivi kwamba ‘alijua’ na ‘kushawishwa kuamini.’ Matokeo yakawa nini? Mazoezi hayo yalitimiza fungu muhimu katika kumfanya awe “mwenye hekima kwa ajili ya wokovu.”—2 Timotheo 1:5; 3:14, 15.
Vivyo hivyo leo, wazazi ambao ‘hawafi moyo katika kufanya lililo bora’ watavuna thawabu nyingi ikiwa ‘hawachoki kabisa.’ (Wagalatia 6:9) Mfalme Solomoni mwenye hekima asema: “Baba yake mwenye haki atashangilia.”—Mithali 23:24.