Jina la Mungu Larudishwa
BAADA ya jina Yehova kuondolewa kwenye Biblia kwa miaka mingi na hata labda kwa karne nyingi, mashahidi wake wa siku hizi ndio dini pekee ya Kikristo ambayo imechukua msimamo imara na kuirudisha tetragramatoni.”a
Maneno hayo yaliyo juu yametolewa kwenye kitabu Jeová dentro do Judaísmo e do Cristianismo (Yehova Katika Dini ya Kiyahudi na Ukristo), kilichoandikwa na Mbrazili Assis Brasil. Lakini huenda swali likatokezwa, Ingawa tafsiri chache za Biblia hutumia jina la Mungu katika namna moja au nyingine, kwa nini dini nyingine zimeliondoa katika Biblia zao? “Jina la Mungu liliondolewa,” asema Brasil, “ama kwa sababu ya ushirikina . . . , ama nia isiyojulikana, ama tamaa ya kukweza jina la Yesu na la mama yake, Mariamu.”
Hata hivyo, kama Bw. Brasil aonyeshavyo kwa usahihi: “Kuondolewa kwa jina [la Mungu] kumesahihishwa kabisa katika lugha ya Kireno na New World Translation of the Holy Scriptures.” Jinsi gani? Kwa njia ya kwamba jina Yehova limerudishwa mahali pake panapofaa kwenye Biblia. Jina Yehova huonekana zaidi ya mara 7,200 katika New World Translation.
Tangu ilipotolewa mara ya kwanza, nakala zaidi ya milioni sita na nusu za tafsiri hii ya kisasa, na ya neno kwa neno katika lugha ya Kireno zimegawanywa. Hivyo, mwandishi mmoja wa habari katika gazeti la Brazili Diário do Nordeste (Gazeti la Kaskazini-Mashariki) alichochewa kuuliza, “Je, wajua kwamba Mungu ana jina?” Kwa sababu ya Biblia hii ya kisasa, mamilioni sasa waweza wakajibu, “Ndiyo. Jina la Mungu ni Yehova.”
[Maelezo ya Chini]
a Katika lugha ya Kiebrania, jina la Mungu huandikwa יהוה. Herufi hizi nne (zinazosomwa kutoka kulia kwenda kushoto) kwa kawaida huitwa Tetragramatoni.