Kulinda Sifa Njema
KUCHUNGUZA kwa makini mchoro mzuri kwaweza kuwa jambo lenye kuthawabisha. Mtu anapouchunguza kwa makini, ataona jinsi msanii alivyotumia brashi mara nyingi sana ili kupaka rangi tofauti-tofauti kwenye turubai.
Vivyo hivyo, sifa njema husitawishwa si kwa tendo moja tu kubwa, bali kwa matendo mengi madogo-madogo yanayofanywa kwa kipindi fulani cha wakati. Naam, sifa yetu husitawishwa hatua kwa hatua kupitia matendo yetu.
Kwa upande mwingine, rangi iliyopakwa mahali pasipofaa yaweza kupunguza thamani ya mchoro. Hivyo ndivyo sifa yetu ilivyo. Mfalme Solomoni mwenye hekima alisema hivi: “Upumbavu wa mtu hupotosha njia yake.” (Mithali 19:3) Sifa yetu nzuri yaweza kuharibiwa na lile lisemekanalo kuwa tendo dogo tu la upumbavu—labda mfoko mkali wa hasira, kunywa vileo kupita kiasi, au tendo moja chafu la kingono. (Mithali 6:32; 14:17; 20:1) Hivyo, ni muhimu kujitahidi kupata sifa njema na kujitahidi sana kuilinda.—Linganisha Ufunuo 3:5.