‘Walimcha Mungu’
WAISRAELI walipokuwa utumwani Misri, wazalisha wa Waebrania Shifra na Pua walikuwa katika hali ngumu sana. Katika jitihada za kudhibiti ongezeko kubwa la watu kutoka nchi za kigeni, Farao aliwaamuru wanawake hao: “Wakati mwazalishapo wanawake wa Kiebrania . . . , ikiwa ni mtoto mwanamume, basi mwueni.”—Kutoka 1:15, 16.
Shifra na Pua ‘walimcha Mungu,’ wakapata ujasiri na ‘wasifanye kama walivyoamriwa na huyo mfalme wa Misri.’ Badala yake, waliwahifadhi hai watoto wa kiume, japo hatua hiyo yenye ujasiri ingehatarisha uhai wao. Yehova “akawatendea mema wale wazalisha,” akawathawabisha kwa matendo yao ya kuokoa uhai.—Kutoka 1:17-21.
Masimulizi haya yanakazia jinsi Yehova anavyothamini wale wanaomtumikia. Yeye angeweza kuona matendo ya Shifra na Pua kuwa huruma ya kibinadamu tu japo yalikuwa yenye ujasiri. Kwani, hakuna mwanamke yeyote mwenye akili timamu awezaye kuua kimakusudi watoto wachanga! Lakini, bila shaka Yehova alifikiria kwamba kwa kuhofu wanadamu watu wengine wamefanya matendo makatili sana. Yeye alijua kwamba wazalisha hawakuchochewa tu na fadhili ya kibinadamu bali pia walichochewa na hofu ya kimungu na ujitoaji wao.
Twashukuru kama nini kumtumikia Mungu ambaye huona matendo yetu ya uaminifu! Ni kweli kwamba labda hakuna mmoja wetu ambaye amekabili jaribu la imani ambalo Shifra na Pua walikabili. Lakini, tunaposimama imara kwa yaliyo sawa—tuwe shuleni, kazini, au katika hali yoyote ile—Yehova hapuuzi upendo wetu wenye uaminifu-mshikamanifu. Badala yake, yeye “huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Ndiyo, “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu na mwaendelea kuhudumu.”—Waebrania 6:10.