Je, Biblia Inaweza Kutusaidia Leo?
“ASILIMIA 1 hivi ya Biblia yote nzima ndiyo inayostahili kusomwa, na sehemu zile nyingine hazifai na zimepitwa na wakati.” Hivyo ndivyo mwanamume mmoja kijana alivyosema. Wengi wangekubaliana naye. Ingawa Biblia yaendelea kuwa kitabu kinachouzwa zaidi ulimwenguni kote, mamilioni ya watu hawaisomi nao hawafahamu mafundisho yake.
Toleo la gazeti la habari la Ujerumani Süddeutsche Zeitung la Krismasi ya mwaka wa 1996 lilieleza kwamba “wasomaji wa [Biblia] wanazidi kupungua. Katika enzi ya sayansi na hali inayoenea ya kufuatia mambo yasiyo ya kidini, wengi huyaona masimulizi ya Biblia kuwa mageni na magumu kueleweka.” Uchunguzi mbalimbali wathibitisha jambo hilo. Uchunguzi mwingine waonyesha kwamba watoto wengi hata hawajui kabisa Yesu ni nani. Katika uchunguzi mmoja, watu wanaopungua nusu ya wale waliohojiwa waliweza kusimulia hadithi za Biblia za mwana mpotevu na Msamaria aliyekuwa jirani mwema.
Kichapo Reformiertes Forum cha Kanisa la Kievanjeli la Uswisi chasema kwamba nchini Uswisi Biblia hazinunuliwi sana kama hapo awali. Hata wale walio na Biblia, mara nyingi hiyo hukaa tu kwenye rafu bila kusomwa. Hali iko vivyo hivyo nchini Uingereza. Kwa mujibu wa uchunguzi mmoja, hata ingawa watu wengi wana Biblia, wengi hawaisomi.
Kwa upande mwingine, mamilioni ya watu ulimwenguni kote wana maoni tofauti kuhusu Biblia. Wanaiona kuwa Neno la Mungu na pia kuwa yenye thamani na yenye manufaa. Hivyo, wao huisoma kwa ukawaida. Mwanamke mmoja kijana aliandika: “Mimi hujitahidi kusoma sura moja au mbili za Biblia kila siku. Nafurahia jambo hilo sana.” Watu hao huzingatia sana yale ambayo Biblia hufundisha, nao hujitahidi kutumia mashauri yake maishani mwao. Wanaamini kwamba Biblia inaweza kuwasaidia katika ulimwengu wa leo wenye taabu.
Wewe waonaje? Je, Biblia haifai siku hizi? Au ni yenye thamani na yenye manufaa? Je, Biblia inaweza kutusaidia leo?