Kukabili Magumu ya Kulea Watoto
LEO ni vigumu sana kwa wazazi kulea watoto, hasa wale walio katika miaka ya ujana. Gazeti la The Gazette la Montreal, Kanada, laripoti kwamba limekuwa “jambo la kawaida kwa vijana” kunywa vileo na kutumia dawa za kulevya. Gazeti hilo lakazia kwamba wazazi wana “daraka la kuwa waangalifu kuona mabadiliko katika tabia ya vijana [wao].”
Wazazi wapaswa kuchunguza mambo gani yawezayo kuonyesha kwamba kijana ana matatizo hayo? Ishara za kimwili, kihisia-moyo, na kijamii, ambazo zilitajwa na shirika la American Academy of Child and Adolescent Psychiatry, zatia ndani uchovu wa daima, mabadiliko ya utu na tabia, kujifungia katika chumba cha kulala kwa muda mrefu kupita kiasi, tabia ya kutaka makabiliano, na kukamatwa kwa kuvunja sheria.
Wazazi wanaweza kuwalindaje watoto wao dhidi ya mambo mabaya kama hayo yenye kudhuru? Dakt. Jeffrey L. Derevensky wa Chuo Kikuu cha McGill, aamini kwamba mawasiliano ya wazi na kusitawisha staha kati ya mzazi na mtoto wakati anapokua, kwaweza kupunguza matatizo baadaye. Gazeti la The Gazette laongezea kusema kwamba hata ingawa tamaa ya kuwa na uhuru mwingi zaidi hutokea wakati wa ujana, vijana bado wanahitaji “mwongozo, msaada, mpango, na upendo kutoka kwa wazazi wao.” Maoni hayo yanafanana na mithali moja ya Biblia isemayo: “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) Mungu huwashauri wazazi wawe vielelezo, rafiki, wawasilianaji, na walimu.—Kumbukumbu la Torati 6:6, 7.