‘Upepo Unapokuwa Dhidi Yetu’
Alipokuwa akieleza jambo lililowapata wanafunzi wa Yesu walipojitahidi sana kuvuka Bahari ya Galilaya kwa mashua, mwandishi wa Gospeli Marko asema kwamba ‘walitaabishwa sana katika kuvuta kwao makasia, kwa maana upepo ulikuwa dhidi yao.’ Yesu alishuhudia hali yao mbaya akiwa ukingoni, naye akatembea kimuujiza juu ya bahari kuwaelekea. Alipopanda kuingia katika mashua pamoja nao, upepo ulipunguka.—Marko 6:48-51.
Mwandishi huyo huyo wa Biblia aliripoti kwamba katika pindi nyingine mapema, ‘kulitokea dhoruba kubwa ya upepo wenye nguvu nyingi.’ Ndipo, Yesu ‘akakemea upepo huo. . . , na upepo ukapunguka, kukawa shwari kubwa.’—Marko 4:37-39.
Ijapokuwa leo hatuna pendeleo la kushuhudia matukio hayo ya kimuujiza, tunaweza kujifunza mengi kutokana nayo. Tukiwa wanadamu wasio wakamilifu wanaoishi katika nyakati za hatari, hatuwezi kuepuka upepo wa majanga. (2 Timotheo 3:1-5) Kwa kweli, nyakati nyingine sisi huenda tukahisi kwamba msononeko unaosababishwa na majaribu ya kibinafsi huwa mkubwa kama dhoruba ya upepo. Lakini kuna kitulizo! Yesu atoa mwaliko huu: “Njoni kwangu, nyinyi nyote mnaomenyeka na kulemezwa mizigo, nami hakika nitawaburudisha nyinyi.”—Mathayo 11:28.
Inapoonekana kwamba ‘upepo uko dhidi yetu,’ twaweza kuwa na ‘shwari kubwa’ moyoni. Jinsi gani? Kwa kutumaini ahadi za Yehova Mungu zisizoshindwa.—Linganisha Isaya 55:9-11; Wafilipi 4:5-7.