Wanadamu—Je, Wao Ni Wanyama Tu wa Hali ya Juu?
“Je, haidhuru tunaamini nini kuhusu asili ya uhai?”
Msichana mmoja mwenye umri wa miaka 16 kutoka Brazili aliuliza swali hilo katika utangulizi wa hotuba yake yenye kichwa “Wanadamu—Je, Wao Ni Wanyama Tu wa Hali ya Juu?” Baada ya mwalimu wake kupokea gazeti la Amkeni! la Juni 22, 1998, lililozungumzia habari hiyo, yeye alimwomba mwanafunzi huyo azungumzie darasa kuhusu suala hilo.
Shahidi huyo mchanga alikazia madhara ambayo yametokezwa na fundisho la mageuzi linalotegemea uteuzi asilia. Kwa mfano, watu wengi huhisi kwamba nadharia ya mageuzi ilifanya wengine wavione vita kuwa sehemu tu ya lile pambano la daima la kusalimika, jambo lililofanya Ufashisti na Unazi usitawi.
Mwanafunzi huyo alionyesha kwamba kuna tofauti kubwa sana kati ya wanadamu na wanyama. Yeye alisema: “Ni wanadamu tu wanaoweza kusitawisha hali ya kiroho. Wanadamu tu ndio hujaribu kujua maana na kusudi la uhai. Wanadamu tu ndio hufikiria kifo, hujishughulisha kujua asili yao, na kutamani kuishi milele. Ni muhimu kama nini kwamba tutumie wakati kufanya uchunguzi zaidi kuhusu asili yetu!”
Mwalimu huyo alisifu hotuba hiyo nzuri. Alisema Shahidi huyo tineja aliweza kuitoa vizuri kwa sababu yeye anapenda kusoma. Msichana huyo anajulikana shuleni kuwa msomaji mwenye bidii wa vichapo vyenye kutegemea Biblia kama Amkeni! na Mnara wa Mlinzi.
Mashahidi wa Yehova huhangaikia kwa moyo mweupe madhara ambayo nadharia ya mageuzi hutokeza katika mioyo na akili ya vijana. Kwa sababu hiyo, kutaniko ambalo msichana huyu anashirikiana nalo liliwatia moyo vijana Mashahidi wawape walimu na wanashule wenzao gazeti la Amkeni! la Juni 22, 1998. Magazeti yapatayo 230 yalipelekwa katika shule mbalimbali jijini. Mkuu wa Idara ya Sayansi katika shule moja aliandikisha gazeti la Amkeni!
Naam, yale tunayoamini kuhusu asili ya uhai yanatuathiri! Kijana huyo na rafiki zake wameonyesha kwamba imani katika Muumba imefanya maisha yao yawe tofauti sana.