Tukio la Pekee-Je, Utakuwepo?
KATIKA siku moja ya kukumbukwa miaka zaidi ya 3,500 iliyopita, Yehova Mungu aliagiza kila nyumba ya Waisraeli waliokuwa watumwa nchini Misri wachinje mwana-kondoo au mbuzi na kunyunyiza damu yake kwenye miimo na vizingiti vya nyumba zao. Usiku huohuo, malaika wa Mungu alipita juu ya nyumba zilizokuwa zimetiwa alama kwa damu lakini akaua wana wa kwanza katika nyumba za Wamisri wote. Kisha Waisraeli wakawekwa huru. Kwenye ukumbusho wa kila mwaka wa tukio hilo, Wayahudi wamesherehekea Sikukuu ya Kupitwa.
Punde tu baada ya Yesu Kristo kumaliza kusherehekea Sikukuu ya Kupitwa pamoja na mitume wake, alianzisha mlo ambao ungewakumbusha kifo chake cha kidhabihu. Aliwapa mitume wake mkate usiotiwa chachu na kusema: “Chukueni, kuleni. Huu wamaanisha mwili wangu.” Kisha akawapa kikombe cha divai na kusema: “Nyweni kutoka hicho, nyinyi nyote; kwa maana hii yamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ inayopaswa kumwagwa kwa niaba ya wengi kwa msamaha wa dhambi.” Yesu pia alisema: “Fulizeni kufanya hili katika ukumbuko wangu.” (Mathayo 26:26-28; Luka 22:19, 20) Hivyo Yesu akawaamuru wafuasi wake wafanye mwadhimisho huo wa kifo chake.
Mwaka huu, ukumbusho wa kila mwaka wa kifo cha Yesu utakuwa Jumatano, Aprili 19, baada ya jua kushuka. Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote watakusanyika jioni hiyo ya pekee ili kuadhimisha Ukumbusho huo kulingana na vile Yesu alivyotaka uadhimishwe. Mnaalikwa kwa uchangamfu mjiunge nasi mkiwa watazamaji. Tafadhali pata habari kutoka kwa Mashahidi wa Yehova wa kwenu juu ya wakati barabara na mahali pa kukutania.