‘Nitaizunguka Madhabahu Yako, Ee BWANA’
“NITANAWA mikono yangu kwa kutokuwa na hatia, na kuizunguka madhabahu yako, Ee BWANA.” (Zaburi 26:6) Mfalme Daudi wa kale alitumia maneno hayo kutangaza ujitoaji wake kwa Yehova. Lakini, kwa nini ‘aliizunguka’ madhabahu ya Yehova, na alifanyaje hivyo?
Kwa habari ya Daudi, kituo cha ibada ya Yehova kilikuwa tabenakulo yenye madhabahu iliyofunikwa kwa shaba, ambayo wakati wa utawala wake ilikuwa Gibeoni, upande wa kaskazini wa Yerusalemu. (1 Wafalme 3:4) Madhabahu hiyo ilitoshana na meta 2.2 tu za mraba, ndogo sana kuliko madhabahu yenye fahari ambayo ingejengwa katika ua wa hekalu la Solomoni.a Na bado, Daudi alifurahia sana tabenakulo na madhabahu yake, ambayo ilikuwa kituo cha ibada ya kweli katika Israeli.—Zaburi 26:8.
Matoleo ya kuteketezwa, dhabihu za ushirika, na matoleo ya ondoleo la hatia zilitolewa kwenye madhabahu, na katika Siku ya Kufunika ya kila mwaka dhabihu zilitolewa kwa niaba ya taifa. Madhabahu na dhabihu zake zina maana kwa Wakristo leo. Mtume Paulo alieleza kwamba madhabahu inawakilisha mapenzi ya Mungu, na kwa kupatana na mapenzi hayo Mungu alikubali dhabihu ifaayo kwa ajili ya ukombozi wa wanadamu. Paulo alisema: “Kwa hayo ‘mapenzi’ yasemwayo sisi tumetakaswa kupitia toleo la mwili wa Yesu Kristo mara moja kwa wakati wote.”—Waebrania 10:5-10.
Kabla tu ya kuhudumu kwenye madhabahu, makuhani walikuwa na desturi ya kunawa mikono kwa maji ili kujitakasa. Kwa kufaa basi, Mfalme Daudi alinawa mikono “kwa kutokuwa na hatia” kabla ya ‘kuizunguka madhabahu.’ Alitenda “kwa ukamilifu wa moyo, na kwa adili.” (1 Wafalme 9:4) Kama hangalinawa mikono kwa njia hiyo, ibada yake—‘kuizunguka madhabahu’—haingalikubalika. Bila shaka, Daudi hakuwa Mlawi na hakuwa na pendeleo la kufanya utumishi wa kikuhani kwenye madhabahu. Ijapokuwa alikuwa mfalme, hata hakukubaliwa kuingia katika ua wa tabenakulo. Lakini, akiwa Mwisraeli mwaminifu, alitii Sheria ya Kimusa na alileta kwa kawaida matoleo yake kwenye madhabahu. Aliizunguka madhabahu kwa maana ya kwamba ibada safi ilikuwa ndiyo jambo la maana zaidi katika maisha yake.
Je, leo tunaweza kufuata mfano wa Daudi? Ndiyo. Sisi pia tunaweza kunawa mikono kwa kutokuwa na hatia na kuizunguka madhabahu ya Mungu tukiweka imani katika dhabihu ya Yesu na, ‘kuwa na mikono safi na moyo mweupe,’ tukimtumikia Yehova kwa moyo wote.—Zaburi 24:4.
[Maelezo ya Chini]
a Madhabahu hiyo ilikuwa meta tisa hivi za mraba.
[Picha katika ukurasa wa 23]
Madhabahu iliwakilisha mapenzi ya Yehova, na kuipitia yeye hukubali dhabihu ifaayo kwa ajili ya ukombozi wa wanadamu