Kudumu Ukiwa Mwaminifu-Mshikamanifu kwa Yehova
UAMINIFU-MSHIKAMANIFU, ujapokuwa nadra sana leo, ni sifa ambayo huwatambulisha watumishi wa Mungu wa kweli, Yehova. Mtu mwaminifu-mshikamanifu hudumu akiwa imara wakati wa majaribu, na thabiti japo kupita kwa wakati. Hebu mfikirie Mfalme mwema Hezekia. “Baada yake hapakuwa na mfano wake katika wafalme wote wa Yuda, wala katika hao waliomtangulia,” Biblia yasema. Ni nini kilichomfanya Hezekia awe tofauti na wengine? “Alishikamana na BWANA,” ingawa alizungukwa na waabudu wa Moleki, mungu asiye wa kweli. Naam, Hezekia “hakuacha kumfuata [Yehova], bali alizishika amri zake.”—2 Wafalme 18:1-6.
Mtume Paulo pia alidumu akiwa mwaminifu-mshikamanifu kwa Yehova. Utumishi wake ulioandikwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo huthibitisha waziwazi kwamba Paulo alikuwa mshikamanifu katika utumishi wake wa nafsi yote kwa Mungu. Alipokaribia kufa, Paulo aliweza kusema hivi: “Nimepigana pigano bora, nimekimbia mwendo hadi mwisho, nimeshika imani.”—2 Timotheo 4:7.
Hezekia na Paulo ni mifano mizuri kama nini! Na tuige imani yao kwa kudumu tukiwa waaminifu-washikamanifu kwa Mungu wetu Mtukufu, Yehova.—Waebrania 13:7.