Kwa Nini Uwe Mwenye Kusamehe?
“WANASAYANSI wameanzisha uchunguzi ambao umeanza kuonyesha kwamba kusamehe kwaweza kuboresha hali ya kihisia-moyo na, huenda pia afya ya kimwili,” linaripoti The Toronto Star, gazeti la habari la Kanada. Ingawa hivyo, Profesa Carl Thoresen wa Chuo Kikuu cha Stanford, Marekani, ambaye ni mtafiti mkuu wa Stanford Forgiveness Project, anasema kwamba “ni watu wachache sana wanaoelewa msamaha ni nini na jinsi unavyofanya kazi.”
Msamaha wa kweli huonwa kuwa sifa muhimu sana ya Ukristo. Ripoti hiyo ya The Toronto Star yafasili sifa hiyo kuwa “kutambua kwamba umekosewa, kutupilia mbali hisia zote za kuchukizwa, na hatimaye kumtendea mkosaji kwa huruma na hata kwa upendo.” Msamaha ni tofauti na kupuuza, kutolea udhuru, kusahau au kukana kosa; wala haumaanishi kujiweka mwenyewe katika hatari ya kutendwa vibaya tena. Ripoti hiyo yasema kuwa msamaha wa kweli ni “kuachilia hasira pamoja na hisia mbaya.”
Wachunguzi wanasema kwamba bado uchunguzi zaidi wahitajiwa kufanywa juu ya manufaa ya kimwili yanayotokana na msamaha. Hata hivyo, wanaripoti kuwa kuna manufaa ya kiakili, kama “kutokuwa na mikazo mingi, hangaiko na mshuko wa moyo.”
Sababu nzuri ya kusamehe inaonyeshwa kwenye Waefeso 4:32, ambalo husema: “Iweni wenye fadhili nyinyi kwa nyinyi, wenye huruma kwa njia nyororo, mkisameheana kwa hiari mtu na mwenzake kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe nyinyi kwa hiari.” Kama ilivyo na mambo mengine mengi, tunasihiwa kuwa waigaji wa Mungu katika kusamehe.—Waefeso 5:1.
Kukataa kuwasamehe wengine ilhali kuna msingi wa kuonyesha rehema kwaweza kuathiri vibaya uhusiano wetu na Mungu. Yehova hutaka tusameheane sisi kwa sisi. Ndipo tuwezapo kumwomba yeye atusamehe.— Mathayo 6:14; Marko 11:25; 1 Yohana 4:11.