Amani ya Ulimwengu Jinsi Gani?
JE, AMANI ya ulimwengu itapatikana hivi karibuni? Wengi walioamini hivyo zamani sasa wanashuku. Ripoti kuhusu matatizo ya wakati ujao, iliyochapishwa katika gazeti la Daily Mail & Guardian la Afrika Kusini, yasema kuwa “matabiri juu ya utaratibu mpya wa kimataifa wa kijamii na kisiasa yaliyotolewa miaka 10 tu iliyopita sasa hayawezi kutumainika.”
Waandikaji hao warejezea matumaini yaliyokuwapo miaka kumi tu iliyopita. Vita Baridi ilikuwa imekoma, na ugomvi kati ya mataifa yenye uwezo mkubwa zaidi ulimwenguni haukuwepo tena. Wengi walidhani kwamba enzi mpya imeanza, na wanadamu wangefaulu kutatua matatizo kama vile umaskini, magonjwa, na masuala ya mazingira. “Matabiri hayo sasa yaonekana kama ndoto tu,” yasema ripoti hiyo. “Vita vipya vimeanza mahali ambapo hata hatukupajua; umaskini waendelea kuongezeka ulimwenguni pote. Mataifa mengine mawili yana silaha za nyuklia. Sifa ya Umoja wa Mataifa imeharibika kabisa kwa sababu limeshindwa kusaidia ifaavyo katika nyakati za hatari zinazotisha hali njema za wanadamu. Mtazamo unabadilika, kwanza watu walitarajia mema yasiyowezekana, sasa wanatarajia mabaya yenye kutisha.”
Wanafunzi wa Biblia wanatambua kwamba hata jitihada za wanadamu ziwe zenye kusifika kadiri gani, haziwezi kufaulu kabisa. Kwa nini? Kwa kuwa, kama Biblia inavyosema, “ulimwengu mzima unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yohana 5:19) Maadamu ulimwengu uko chini ya uongozi wa Shetani, hautapata kuwa Paradiso kama Mungu alivyokusudia alipouumba.
Hata hivyo, kuna tumaini. Yehova Mungu anaahidi kuleta amani ulimwenguni, si kwa kurekebisha mfumo huu wa mambo, bali kwa kuleta “dunia mpya” ambamo katika hiyo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Naam, kupitia Ufalme wa Mungu, sayari yetu itageuzwa kuwa mahali penye utulivu na furaha, ambapo maisha na kazi zitakuwa zikifurahisha daima wanadamu wote watiifu. Zaidi ya hayo, Mungu anaahidi ‘kufuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe.’ Chanzo cha ahadi hizo si matabiri yasiyotegemeka ya wanadamu. Badala yake ni Neno kamilifu la Muumba asiyeweza kusema uwongo.—Ufunuo 21:4; Tito 1:2.