Je, Dini Italeta Amani ya Ulimwengu?
KUANZIA Agosti 28 hadi Agosti 31, 2000, zaidi ya wawakilishi 500 kutoka nchi 73 walikutanika New York City. Walikutanika kwenye jengo la Umoja wa Mataifa ili kuhudhuria “Mkutano wa Milenia wa Viongozi wa Kidini na Kiroho Kuhusu Amani ya Ulimwengu.” Viongozi hao, ambao wengi wao walikuwa wamevalia vilemba, kanzu za manjano, kofia zenye manyoya ya ndege, au majoho meusi marefu, waliwakilisha dini nyingi mbalimbali. Baadhi ya hizo zilikuwa Dini ya Bahai, Ubudha, Uhindu, Uislamu, Ujaini, Dini ya Kiyahudi, Dini ya Shinto, Dini ya Sikh, Dini ya Tao, Uzoroasta, na dini za Jumuiya ya Wakristo.
Wajumbe hao walikutana kwenye jengo la Umoja wa Mataifa kwa siku mbili za kwanza za mkutano huo wa siku nne. Hata hivyo, mkutano huo haukupangwa wala kugharimiwa na Umoja wa Mataifa bali na mashirika mbalimbali. Hata hivyo, Umoja wa Mataifa na viongozi wa kidini walisema juu ya umuhimu wa kufanya kazi kwa umoja ili kumaliza umaskini, ukabila, matatizo ya mazingira, vita, na silaha zinazoweza kuua watu wengi.
Wajumbe hao walitia sahihi hati yenye kichwa “Wajibu wa Kuleta Amani ya Ulimwengu.” Hati hiyo ilisema kwamba wale walioitia sahihi “wa[nge]unga mkono Umoja wa Mataifa . . . katika jitihada ya kuleta amani,” huku ikikubali kwamba “mara kwa mara [ujeuri na vita] hutokezwa na dini.” Hata hivyo, hakukuwa na maazimio hususa kuhusu jinsi ambavyo jambo hilo lingetimizwa.
Katika siku ya pili, Bawa Jain, katibu mkuu wa mkutano huo, alimaliza maneno ya ufunguzi kwa kueleza kwamba miaka kadhaa iliyopita alikuwa ameona mchoro fulani kwenye jengo la Umoja wa Mataifa. Mchoro huo ulionyesha mwanamume aliyekuwa mrefu kuliko jengo la Umoja wa Mataifa. Alikuwa akigonga jengo hilo kana kwamba anabisha mlango. Maneno haya yalikuwa yameandikwa chini ya mchoro: “Mfalme wa Amani.” Bw. Jain alisema: “Mara nilipouona [mchoro huo] niliguswa hisia. Niliwauliza watu mbalimbali maana [yake]. Leo, nadhani ninajua. Kukutanika kwa nyinyi nyote hapa, viongozi wa kiroho na wa kidini wa ulimwengu, kwanidhihirishia kwamba [nyinyi] ni mfalme wa amani abishaye mlango wa Umoja wa Mataifa.”
Hayo si maoni ya Biblia. Biblia yaonyesha kwamba Mfalme wa Amani ni Yesu Kristo. Yeye ataleta amani duniani kote, si kupitia jitihada za viongozi wa kisiasa wala viongozi wa kidini wa ulimwengu huu, bali kupitia Ufalme wa Mungu. Ni Ufalme huo—serikali ya mbinguni ya Mungu—ambao utafaulu kuunganisha wanadamu watiifu na kufanya mapenzi ya Mungu yatimizwe duniani.—Isaya 9:6; Mathayo 6:9, 10.