“Jeraha Utiwazo na Rafiki”
MTUME Paulo aliona uhitaji wa kutoa shauri la kusahihisha Wakristo wa karne ya kwanza huko Galatia. Yaelekea alitaka kuzuia uchungu wa moyo, alipouliza hivi: “Hivyo basi, je, nimekuwa adui yenu kwa sababu nawaambia nyinyi kweli?”—Wagalatia 4:16.
Paulo hakuwa adui yao kwa ‘kuwaambia kweli.’ Kwa hakika, alikuwa akitenda kupatana na kanuni hii ya Biblia: “Jeraha utiwazo na rafiki ni amini.” (Mithali 27:6) Paulo alijua kwamba watu fulani wenye kiburi wangeudhika. Hata hivyo, alijua kwamba kutompa mkosaji nidhamu anayohitaji kungemaanisha kwamba mkosaji huyo amenyimwa upendo wa Yehova Mungu. (Waebrania 12:5-7) Kwa hiyo, Paulo akiwa rafiki mwaminifu na mwenye nia njema, alitaka kunufaisha kutaniko kwa muda mrefu ndiyo sababu hakusita kutoa shauri lenye kusahihisha.
Leo, Mashahidi wa Yehova wanatimiza utume wao wa ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, wakiwafundisha kushika mambo yote ambayo Yesu Kristo aliamuru.’ Wafanyapo hivyo, Wakristo hao wa kweli hawaridhiani kweli za Biblia zinazofunua na kushutumu mafundisho yasiyo sahihi na mwenendo usio wa Kikristo. (Mathayo 15:9; 23:9; 28:19, 20; 1 Wakorintho 6:9, 10) Badala ya kuwa maadui wanaokataliwa, wanaonyesha upendezi wa marafiki wa kweli.
Akiwa na ufahamu uliopuliziwa na Mungu, Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Mwenye haki na anipige, itakuwa fadhili; anikemee, itakuwa kama mafuta kichwani; kichwa changu kisikatae.”—Zaburi 141:5.