Maswali Kutoka kwa Wasomaji
Danieli alikuwa wapi wakati Waebrania watatu walipojaribiwa mbele ya sanamu kubwa iliyosimamishwa na Nebukadneza kwenye uwanda wa Dura?
Biblia haisemi alikuwa wapi, kwa hiyo leo hakuna mtu awezaye kusema kwa uhakika Danieli alikuwa wapi wakati wa jaribu hilo.
Watu wengine wamedokeza kwamba cheo cha Danieli serikalini au mapendeleo ya pekee aliyopewa na Nebukadneza yalikuwa ya juu kuliko ya Shadraka, Meshaki, na Abednego, kwa hiyo Danieli hakuhitajika kwenda kwenye uwanda wa Dura. Andiko la Danieli 2:49 linaonyesha kwamba kwa muda fulani yeye alikuwa na cheo cha juu kuliko wenzake watatu. Lakini hatuwezi kuthibitisha kwamba jambo hilo ndilo lililofanya asihitajike kukusanyika na wengine mbele ya ile sanamu.
Wakijaribu kueleza ni kwa nini Danieli hakuwepo, watu wengine wamesema kwamba huenda alikuwa ameenda kufanya kazi fulani ya kiserikali au alikuwa mgonjwa na hivyo hakuweza kuhudhuria. Lakini Biblia haisemi hivyo. Kwa vyovyote, Danieli alikuwa na sababu nzuri ya kutokuwepo la sivyo maafisa wa Babiloni wenye wivu wangekuwa na sababu ya kumshtaki. (Danieli 3:8) Kabla na baada ya tukio hilo, Danieli alijithibitisha kuwa mtu mwaminifu, mwenye uaminifu-mshikamanifu kwa Mungu licha ya magumu aliyokabili. (Danieli 1:8; 5:17; 6:4, 10, 11) Kwa hiyo, ingawa Biblia haisemi ni kwa nini Danieli hakuwepo kwenye uwanda wa Dura, tunaweza kuwa na uhakika kwamba alikuwa mwaminifu kabisa kwa Yehova Mungu.—Ezekieli 14:14; Waebrania 11:33.