Kazi Bora Humtukuza Mungu
WAKRISTO wa kweli humtukuza Mungu kwa mwenendo wao mzuri na kazi zao nzuri. (1 Petro 2:12) Twaweza kufahamu jambo hilo kwa kufikiria mambo yaliyotukia nchini Italia miaka ya karibuni.
Mnamo Septemba 1997, tetemeko kubwa la dunia lilikumba sehemu mbalimbali za Marche na Umbria na kuharibu nyumba zipatazo 90,000. Mashahidi wa Yehova walienda mara moja kuwasaidia waumini wenzao na watu wengine. Walitoa trela, mifuko ya kulalia, meko, jenereta, na vifaa vingine vilivyohitajika. Jitihada hizo za kuandaa msaada zilionekana waziwazi.
Gazeti Il Centro liliripoti hivi: “Mashahidi wa Yehova kutoka Roseto [katika wilaya ya Teramo] ndio waliokuwa wa kwanza kuleta msaada katika maeneo yaliyokumbwa na tetemeko . . . Mbali na kukutana mara kwa mara ili kusali, watu walio waaminifu kwa Yehova hufanya kazi inayofaa ya kuwasaidia wanaoteseka, bila kujali watu hao ni wa dini gani.”
Meya wa Nocera Umbra, mojawapo ya miji iliyoharibiwa vibaya na tetemeko hilo, aliwaandikia Mashahidi hivi: ‘Nawashukuru sana kwa msaada mliowapa watu wa Nocera. Nina hakika kwamba raia wote wa Nocera wangesema vivyo hivyo.’ Isitoshe, Wizara ya Mambo ya Ndani ililipatia Congregazione Cristiana dei Testimoni di Geova (Kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova) cheti cha sifa njema na nishani “ili kutambua kazi waliyofanya na bidii iliyoonyeshwa katika kazi hiyo ya msaada wa dharura katika maeneo ya Umbria na Marche.”
Mnamo Oktoba mwaka wa 2000, furiko kubwa sana lilikumba eneo la Piedmont kaskazini mwa Italia. Kwa mara nyingine tena, Mashahidi walijiandaa mara moja kupeleka msaada huko. Pia kazi hiyo nzuri ilionekana wazi. Mkoa wa Piedmont uliwapa bamba la kumbukumbu kwa ajili ya “kazi yao yenye thamani ya kujitolea kusaidia watu wa Piedmont waliokumbwa na furiko.”
Yesu Kristo aliwaagiza hivi wanafunzi wake: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu, ili wapate kuona kazi zenu bora na kumpa utukufu Baba yenu aliye katika mbingu.” (Mathayo 5:16) Mashahidi wa Yehova hawajitukuzi bali wao hufurahia kumtukuza Mungu kwa kufanya ‘kazi bora’ za kuwasaidia majirani wao kiroho na katika njia nyinginezo.