Wana Hekima Pia
METHALI moja huko Nigeria husema, “Watu wazima wana hekima, lakini watoto wana hekima pia.” Edwin, mzee Mkristo wa kutaniko la Kikristo huko Nigeria aligundua kwamba mithali hiyo ni ya kweli.
Siku moja, Edwin alikuta kisanduku cha chuma chini ya dawati lake nyumbani.
“Kisanduku hiki ni cha nani”? Edwin akawauliza watoto wake watatu.
“Ni changu,” Emmanuel, mwenye umri wa miaka minane, akajibu. Aliongeza kusema bila kusita kwamba kisanduku hicho cha chuma chenye kutu na ukubwa wa sentimeta 12 mraba, ambacho kilikuwa na kishimo juu, kilikuwa cha kuweka michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote ya Mashahidi wa Yehova. “Kwa kuwa siendi kwenye Jumba la Ufalme kila siku,” akaeleza, “niliamua kutengeneza kisanduku ili niwe nikiweka pesa zangu za chakula cha mchana nisipozitumia.”
Babake Emmanuel alikuwa na kisanduku nyumbani cha kuweka akiba ya pesa ili kuhudhuria kusanyiko la wilaya linalofanywa kila mwaka. Lakini kwa sababu ya jambo fulani la dharura lililotokea katika familia, walitumia pesa hizo. Ili kuhakikisha kwamba mchango wake haungetumiwa kwa jambo lingine, Emmanuel alipeleka kisanduku hicho kwa muunganisha-vyuma fulani ili akifunge. Alipojua ni kwa nini Emmanuel alihitaji kisanduku hicho, muunganisha-vyuma huyo alimtengenezea kisanduku kwa mabaki ya vyuma. Michael, nduguye Emmanuel mwenye umri wa miaka mitano, pia aliomba atengenezewe kisanduku.
Kwa kushangazwa na kitendo hicho cha watoto wake, Edwin aliwauliza ni kwa nini walitengenezesha visanduku hivyo. Michael alijibu: “Ninataka kuchanga!”
Wazazi wao hawakujua kwamba Emmanuel, Michael, na Uchei, dada yao mwenye umri wa miaka tisa, walikuwa wakiweka kiasi fulani cha pesa ambazo hawakutumia kununua chakula chao cha mchana kwenye visanduku hivyo. Walipata wapi wazo hilo? Mara tu watoto hao walipoweza kujua thamani ya pesa, wazazi wao waliwafundisha kuweka kiasi fulani cha pesa katika sanduku la michango kwenye Jumba la Ufalme. Kwa kweli watoto hao walifanya kama walivyojifunza.
Visanduku hivyo vilipojaa, vilikatwa ili kufunguliwa. Akiba yao ilikuwa dola 3.13 (za Marekani)—kiasi kikubwa cha pesa katika nchi ambako wastani wa mapato kwa mwaka ni dola mia chache tu. Michango hiyo ya hiari hutegemeza kazi ya kuhubiri ya Mashahidi wa Yehova inayofanywa katika nchi 235 ulimwenguni pote.