Alikuwa Mzee Lakini Hakuwa Mpweke
KWA SABABU ya uzee, wengi hulemaa na kutengwa na watu. Haikuwa hivyo kwa Fernand Rivarol, aliyekufa akiwa na umri wa miaka 95 huko Geneva, Uswisi. Alikuwa anaishi peke yake kwa kuwa mke wake alikuwa amekufa na binti yake alikuwa ameolewa na kuondoka nyumbani. Ingawa mara nyingi hangetoka nyumbani, hakuwa mpweke. Sikuzote aliketi sebuleni akizungumza na watu mambo ya kiroho kupitia simu.
Ingawa Fernand alifurahia maisha yake, kuna wakati ambapo hangeweza kutoka nyumbani kabisa. Kwa nini? Mara tu baada ya Fernand na mke wake kuwa Mashahidi wa Yehova wenye bidii mwaka wa 1939, Vita vya Pili vya Ulimwengu vilianza huko Ulaya. Fernand alishikilia kanuni ya Biblia ya kutomuumiza mtu yeyote. Kwa sababu hiyo, alifutwa kazi na akafungwa gerezani mara nyingi. Kwa jumla, alitengwa na mke na binti yake mdogo kwa miaka mitano na nusu.
Alipokumbuka mambo hayo, Fernand alisema: “Watu wengi waliona kana kwamba niliacha kazi nzuri na kuacha kuitegemeza familia yangu. Watu walinichukia na kunitendea kama mhalifu. Hata hivyo, ninapofikiria miaka hiyo ya shida, ninakumbuka sana jinsi Yehova alivyotutegemeza na kutusaidia. Miaka mingi imepita tangu wakati huo, lakini imani yangu kwa Yehova bado ni thabiti kama ilivyokuwa wakati huo.”
Imani hiyo ilimchochea Fernand kutumia simu kuwaambia wengine tumaini lake linalotegemea Maandiko. Alipopata mtu anayependezwa na ujumbe wake, alimtumia vichapo vya Biblia. Baadaye, alimpigia simu mtu huyo ili kujua ikiwa alifurahia kuvisoma. Wakati mwingine watu walimwandikia barua za shukrani, na jambo hilo lilimfurahisha sana.
Huenda ukakutana na mtu fulani kama Fernand katika eneo lenu. Tafadhali msikilize ili ujue yale anayoamini. Mashahidi wa Yehova wako tayari sikuzote kukuambia mambo wanayoamini.