“Kwa Nini Tupo Hapa?”
PINDI moja Elie Wiesel, mshindi wa Tuzo la Nobeli ambaye pia ni mwokokaji wa Maangamizi ya Nazi, alisema kwamba swali hilo “ndilo swali muhimu zaidi ambalo mwanadamu anapaswa kutafakari.” Swali gani? Ni hili, “Kwa nini tupo hapa?”
Je, umewahi kutafakari kuhusu swali hilo? Watu wengi wamefanya hivyo, lakini hawajapata jibu. Akijaribu kueleza ni nini lililo kusudi la maisha, mwanahistoria Mwingereza, Arnold Toynbee aliandika: “Lengo la kweli la mwanadamu ni kumtukuza Mungu na kupata furaha milele kutokana Naye.”
Inapendeza kwamba zaidi ya miaka elfu tatu iliyopita, mwanamume mwingine aliyejulikana kwa kuchunguza maisha kwa makini, tayari alikuwa amejibu swali hilo. Mfalme Sulemani mwenye hekima alisema hivi: “Huu ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.”—Mhubiri 12:13.
Kanuni hiyo ya msingi iliungwa mkono na Mwana wa Mungu, Yesu Kristo. Alipokuwa duniani, Yesu alijitahidi awezavyo kumtukuza Baba yake wa mbinguni. Kumtumikia Muumba wake kulifanya maisha ya Yesu yawe na kusudi. Kulimtia nguvu na kumwimarisha, hivi kwamba akasema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma.”—Yohana 4:34.
Hivyo, kwa nini tupo hapa? Kama Yesu, Sulemani, na watumishi wengine wengi wa Mungu, tunaweza kuwa na maisha yenye kusudi kwelikweli na furaha ya kudumu ikiwa tutafanya mapenzi ya Mungu. Je, ungependa kujua mengi zaidi kuhusu jinsi ya kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli”? (Yohana 4:24) Mashahidi wa Yehova katika eneo lenu watafurahi kukusaidia kupata jibu la swali hili, “Kwa nini tupo hapa?”