Umuhimu wa Kuandika Katika Israeli la Kale
JE, UMEWAHI kusoma mashairi mawili yanayojulikana sana kutoka Ugiriki ya kale (Iliad au Odyssey)? Inasemekana kwamba mashairi hayo yalitungwa katika karne ya tisa au ya nane K.W.K. Mashairi hayo yanahusiana kwa njia gani na Biblia, ambayo ilianza kuandikwa karne nyingi mapema? Kitabu kimoja (The Jewish Bible and the Christian Bible) kinasema hivi: “Katika Biblia, maneno kuandika na hati zilizoandikwa yanapatikana angalau mara 429. Hilo ni jambo la maana sana tukikumbuka kwamba mashairi ya Iliad yanataja neno kuandika mara moja tu na mashairi ya Odyssey hayataji hata mara moja.”
Kitabu kimoja (The Oxford Encyclopedia of Archaeology in the Near East) kinaeleza kwamba “katika Israeli la kale inaonekana kwamba kuandika kulikuwa sehemu ya maana sana katika dini.” Kwa mfano, agano la Sheria liliandikwa na baadaye likasomwa mbele ya watu kwa ukawaida, yaani, mbele ya wanaume wote, wanawake, na watoto. Pia, watu walisoma na kujifunza agano hilo wakiwa katika vikundi au peke yao. Baada ya kuchunguza mambo fulani ya Sheria hiyo, Alan Millard, mhadhiri mkuu katika Chuo Kikuu cha Liverpool, anakata kauli hii: “Ni wazi kwamba kusoma na kuandika kulionwa kuwa muhimu sana kwa kila Mwisraeli.”—Kumbukumbu la Torati 31:9-13; Yoshua 1:8; Nehemia 8:13-15; Zaburi 1:2.
Mtume Paulo anaeleza jinsi Wakristo wanavyopaswa kuona maandishi hayo matakatifu: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” Je, wewe binafsi unaonyesha kwamba unaithamini Biblia kwa kuisoma kwa ukawaida?—Waroma 15:4.