Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu
Kwa Nini Wakristo Hubatizwa?
Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.
1. Ubatizo wa Kikristo unamaanisha nini?
Ubatizo ni njia ya kumwomba Mungu akuruhusu uwe na uhusiano wa karibu naye. Hivyo, Mkristo hapaswi kubatizwa akiwa mtoto mchanga, bali anapokuwa na umri wa kutosha kujifunza kumhusu Mungu na kuwa mwanafunzi wa Yesu. (Matendo 8:12; 1 Petro 3:21) Tunakuwa wanafunzi wa Yesu tunapojifunza na kufanya mambo aliyoamuru.—Soma Mathayo 28:19, 20.
Katika nyakati za mitume wa Yesu, watu wengi walichukua hatua bila kukawia kujifunza kumhusu Mungu na Yesu. Kwa mfano, mwanamume fulani alipotambua kwamba inawezekana kupata wokovu kupitia kifo cha Yesu, alichukua hatua mara moja na kuwa mfuasi wake. Leo, watu wengi wenye mioyo minyoofu wameamua kuwa wafuasi wa Yesu.—Soma Matendo 8:26-31, 35-38.
2. Kwa nini Yesu alibatizwa?
Yesu alikuwa na umri wa miaka 30 hivi Yohana Mbatizaji alipombatiza ndani ya maji ya Mto Yordani. Ubatizo wa Yesu ulionyesha uamuzi wake wa kufanya mapenzi ya Mungu. (Waebrania 10:7) Daraka hilo lilitia ndani kutoa uhai wake kuwa dhabihu kwa ajili ya dhambi za wanadamu. Hata kabla ya kuja duniani, sikuzote Yesu alimpenda na kumtii Baba yake, Yehova.—Soma Marko 1:9-11; Yohana 8:29; 17:5.
3. Kwa nini Mkristo anapaswa kubatizwa?
Hali yetu ni tofauti na ya Yesu, kwa sababu tunazaliwa tukiwa watenda dhambi. Hata hivyo, kifo cha kidhabihu cha Yesu kinatuwezesha kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. (Waroma 5:10, 12; 12:1, 2) Kinatuwezesha kuwa watu wake tukiwa sehemu ya familia yake. (2 Wakorintho 6:18) Tunawezaje kupata pendeleo hilo? Kupitia sala ya kibinafsi, mtu anajitoa kumtumikia Yehova, na kuweka nadhiri ya kufanya mapenzi ya Mungu katika maisha yake yote. Baada ya kufanya hivyo, anabatizwa hadharani ili kuonyesha kwamba amejitoa kumtumikia Mungu.—Soma Mathayo 16:24; 1 Petro 4:2.
4. Unawezaje kujitayarisha kwa ajili ya ubatizo?
Mashahidi wa Yehova hujifunza Biblia na mtu yeyote anayetaka kumkaribia Mungu. Kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kikristo, kutaimarisha upendo wako kwa Mungu na imani yako kumwelekea. Pia, kutakusaidia kusitawisha mtazamo unaofaa na tabia nzuri. Kuonyesha upendo, imani na sifa nyingine zinazompendeza Mungu kutakusaidia kuishi kulingana na nadhiri yako ya kumtumikia Yehova milele.—Soma Yohana 17:3; Waebrania 10:24, 25.
Kwa habari zaidi ona sura ya 18 ya kitabu, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.