Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w12 11/1 kur. 8-9
  • Swali la 3: Kwa Nini Mungu Anaruhusu Niteseke?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Swali la 3: Kwa Nini Mungu Anaruhusu Niteseke?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
  • Habari Zinazolingana
  • Biblia Inasema Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2017
  • Yaliyomo
    Amkeni!—2020
  • Kuteseka Kuteseka
    Amkeni!—2015
  • Ikiwa Muumba Anajali, Mbona Wanadamu Wanateseka Sana?
    Je, Kuna Muumba Anayekujali?
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
w12 11/1 kur. 8-9

SWALI LA 3: Kwa Nini Mungu Anaruhusu Niteseke?

BABA ya Ian alikuwa mlevi kupindukia. Ingawa Ian hakukosa vitu alivyohitaji, alikosa utegemezo wa kihisia ambao alitamani kupata kutoka kwa baba yake. Ian anasema: “Sikumpenda sana, hasa kwa sababu ya tabia yake ya ulevi na jinsi alivyomtendea mama yangu.” Ian alipoendelea kukua, alianza kuwa na shaka kama kuna Mungu. “Nilijiuliza, ‘Ikiwa kuna Mungu kwa nini anaruhusu watu wateseke?’”

Kwa nini tuulize swali hilo?

Ingawa huenda usiwe na matatizo mengi maishani, unaweza kukasirika unapoona watu wasio na hatia wakiteseka kwa sababu ya ukosefu wa haki. Hata hivyo, kama Ian, unaweza kujiuliza kwa nini watu huteseka unapokabiliana na matatizo au mtu unayempenda anapokuwa mgonjwa au kufa.

Watu fulani wanafikiri jibu ni nini?

Watu fulani wanaamini kwamba Mungu anaruhusu kuteseka ili kutufundisha kuwa wanyenyekevu na wenye huruma. Wengine wanafikiri kwamba watu wanateseka katika maisha haya kwa sababu ya dhambi walizofanya katika maisha ya zamani.

Majibu hayo yanamaanisha nini?

Mungu hajali anapoona wanadamu wakiteseka, na hivyo ni vigumu kwetu kumpenda. Mungu ni mkatili.

Biblia inafundisha nini?

Biblia inaeleza waziwazi kwamba Mungu hapaswi kulaumiwa kwa sababu ya kuteseka kwa wanadamu. “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Hata wazo la kwamba Mungu ndiye wa kulaumiwa kwa sababu ya kuteseka, halipatani na jinsi Biblia inavyofafanua utu wake. Jinsi gani?

Moja kati ya sifa kuu za Mungu ni upendo. (1 Yohana 4:8) Ili kukazia jambo hilo, Biblia inamtaja Mungu akiwa na hisia kama za mama anayenyonyesha. “Je, mke anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya hivi kwamba asimhurumie mwana wa tumbo lake?” Mungu anauliza. “Hata hawa wanawake wanaweza kusahau, lakini mimi mwenyewe sitakusahau wewe.” (Isaya 49:15) Je, unaweza kumwazia mama mwenye upendo akimwumiza mtoto wake kimakusudi? Kinyume cha hilo, mzazi mwenye kujali, atajitahidi kupunguza mateso yanayompata mtoto wake. Vivyo hivyo, Mungu hasababishi watu wasio na hatia wateseke.—Mwanzo 18:25.

Hata hivyo, watu wasio na hatia wanateseka. Huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa Mungu anatujali na ni mwenye uwezo, kwa nini haondoi mambo yanayosababisha kuteseka?’

Mungu ana sababu nzuri za kuruhusu mateso yaendelee. Fikiria sababu moja: Mara nyingi watu ndio huwasababishia wenzao mateso. Watu wengi ambao ni wachokozi na wakatili wanaowaumiza wengine hawataki kubadili tabia zao. Hivyo, ili Mungu aondoe chanzo kikuu cha mateso, atalazimika kuwaangamiza watu hao.

Akifafanua kwa nini Mungu hajawaangamiza watu wanaotenda mabaya, mtume Petro aliandika: “Yehova hakawii kuhusiana na ahadi yake, kama watu fulani wanavyoona kukawia, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (2 Petro 3:9) Subira ya Yehova Mungu inaonyesha utu wake wenye upendo na huruma.

Hata hivyo, hivi karibuni Yehova Mungu atachukua hatua. ‘Atawalipa dhiki wale wanaofanya dhiki.’ Wale wanaosababisha mateso isivyo haki “watahukumiwa adhabu ya uharibifu wa milele.”—2 Wathesalonike 1:6-9.

Ian, aliyetajwa mapema, alipata majibu yenye kuridhisha kwa maswali yake kuhusu kuteseka. Mambo aliyojifunza yalibadili mtazamo wake kuhusu maisha. Soma simulizi lake katika ukurasa wa 13 wa gazeti hili.

Ili ujue zaidi kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka na hatua atakayochukua, ona sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Unaweza kukipakua kwenye Tovuti ya www.jw.org/sw

Yesu Alisema Nini Kuhusu Kuteseka?

Yesu hakumlaumu Mungu kwa sababu ya mateso yaliyompata. Badala yake alifanya mambo yafuatayo.

Yesu alionyesha kwamba Mungu hawaadhibu watu wasio na hatia kwa kuwasababishia mateso. Yesu aliwaponya wagonjwa, vilema, na vipofu. (Mathayo 15:30) Miujiza aliyofanya inatufundisha mambo mawili muhimu: Kwanza, Yesu alitumia nguvu za Mungu kupunguza mateso bali si kuyasababisha. Pili, Yesu hakuwaponya watu bila huruma. Alipowaona watu wakiteseka, ‘aliwasikitikia.’ (Mathayo 20:29-34) Yesu alionyesha kikamili hisia za baba yake kuhusu kuteseka. Kwa hiyo, kutokana na maneno na matendo ya Yesu, tunajifunza kwamba Mungu anahuzunishwa na mateso anayoona na anatamani kuyaondoa.—Yohana 14:7, 9.

Yesu alitaja chanzo cha mateso mengi yanayowapata wanadamu, yaani, Shetani Ibilisi. Yesu alisema: “Huyo alikuwa muuaji alipoanza.” (Yohana 8:44) Yesu pia alisema kwamba Shetani Ibilisi ni “mtawala wa ulimwengu” na ndiye “anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.”—Yohana 12:31; Ufunuo 12:9.

Yesu alitupatia tumaini kwamba kuna wakati ambapo kuteseka kote kutakwisha. Aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Baba yetu uliye mbinguni, . . . Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Ufalme wa Mungu utakapokuja duniani watu hawatateseka tena, kama ilivyo mbinguni ambako hakuna mateso.

Katika ufunuo aliompa Yohana, Yesu alieleza jinsi maisha yatakavyokuwa kwa wale watakaoishi chini ya Ufalme wa Mungu. Wakati huo, Mungu “atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 1:1; 21:3, 4.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki