Matakwa kwa Mhudumu Mpya na Pia Yule Aliye na Ujuzi
1 Mtunga-zaburi Daudi aliuliza: “BWANA [Yehova, New World Translation], ni nani atakayekaa katika hema yako? Ni nani atakayefanya maskani yake katika kilima chako kitakatifu?” Kwa maneno mafupi yaliyochaguliwa vizuri, Daudi alijibu: “Ni mtu aendaye kwa ukamilifu, na kutenda haki. Asemaye kweli.” (Zab. 15:1, 2) Matakwa hayo hayajabadilika. Leo wale wote wanaokuja kuabudu katika kutaniko la Kikristo lazima waache mazoea ya ukosefu wa adili na ulevi. Hakuna nafasi miongoni mwa watu wa Yehova kwa wale wenye ugomvi, walio na hasira kali, au wenye kusema uongo. Tuwe sisi ni wahudumu wapya au walio na ujuzi, ni lazima tuwe waaminifu katika kutimiza viwango vya juu vilivyomo katika Neno la Mungu.—Gal. 5:19-21.
2 Wapya wengi wanashirikiana na tengenezo la Yehova. Wazee kwa vijana wamebadili kufikiri kwao ili wapatanishe njia yao ya maisha na matakwa ya Mungu. Mvulana mmoja katika Amerika ya Kusini alikua bila mwongozo wa wazazi na akasitawisha matatizo magumu ya kiutu. Alipofika umri wa miaka 18, alizoelea dawa za kulevya na akawa tayari amefungwa gerezani kwa kuiba ili kuendeleza tabia hiyo. Kupitia funzo la Biblia, aliacha kushirikiana na mashirika yake ya zamani, akapata marafiki wapya miongoni mwa Mashahidi wa Yehova, na hatimaye akaweka maisha yake wakfu kwa Mungu.
3 Vivyo hivyo, sisi pia twapaswa kuazimia kumpendeza Mungu katika mwenendo wetu wote, “katika haki na utakatifu wa kweli.” (Efe. 4:24) Tuna wajibu wa ‘kuvua kabisa utu wa kale, pamoja na matendo yake’ na ‘kuvaa utu mpya, unaofanywa upya kupitia ujuzi sahihi’ ili kubaki katika tengenezo la Mungu lililo kama mlima.—Kol. 3:9, 10.
4 Neno la Mungu, Athari Yenye Nguvu: Utu wa Yehova kama ufunuliwavyo kwetu kupitia Biblia waweza kuathiri vizuri kufikiri kwetu na matendo yetu. (Rum. 12:2) Neno lake lina nguvu ya kubadili akili na kutafuta mioyo. (Ebr. 4:12) Maandiko yaliyopuliziwa roho hutufundisha kwamba mapenzi ya Yehova hututaka tuishi maisha yenye unyoofu kiadili, tushiriki kikamili katika huduma ya peupe, na tusipuuze mikutano ya Kikristo.
5 Katika nyakati hizi zilizo ngumu kushughulika nazo, mibano inayoongezeka yaweza kumshawishi Mkristo kuvunja sheria za Mungu. Funzo la kibinafsi, funzo la familia, mikutano ya kutaniko, au huduma vikipuuzwa, hata Mkristo aliyekuwa mwenye nguvu wakati mmoja anaweza kupeperushwa kutoka kwa imani, labda kuangukia mwenendo mbaya. Hiyo ndiyo sababu Paulo alimwandikia Timotheo hivi: “Jitunze nafsi yako [daima, NW], na mafundisho yako” na, “Yafahamu [daima, NW] hayo nisemayo.”—1 Tim. 4:16; 2 Tim. 2:7.
6 Tuwe wapya au tumekomaa kwa miaka mingi ya ujuzi, ni lazima tukazie wazi akilini matakwa ya Mungu, tuwe wenye usawaziko kamili katika huduma, na kudumisha tumaini letu lenye nguvu ikiwa uhai wetu utahifadhiwa. (1 Pet. 1:13-16) Kutii matakwa ya Mungu yenye uadilifu kila siku ni muhimu sana.
7 Weka uwe mradi wako kuwa katika utumishi wa shambani katika mwezi huu wa mwisho wa mwaka wa utumishi wa 1993. Azimia kuwasaidia wengine wakue katika imani na uongeze utendaji katika huduma ya shambani. (Rum. 1:12) Weka akili yako kwa mambo yanayofaa kwa kuwa na funzo la kibinafsi, funzo la familia, na kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. (Flp. 4:8) Jitihada zako za kumpendeza Mungu na kuishi kulingana na matakwa yake hazitapuuzwa.—Kol. 3:23, 24.