Ukumbusho wa Ulimwenguni Pote wa Kifo cha Kristo
1 Yehova ametupatia kwa wingi zawadi nyingi. Jumla ya wema wake na fadhili-upendo yake yafafanuliwa waziwazi kuwa “zawadi yake ya bure isiyoelezeka.” Naam, “fadhili isiyostahiliwa ya Mungu” ni ya ajabu sana hivi kwamba yapita uwezo wetu kuifafanua.—2 Kor. 9:14, 15.
2 Zawadi Yake Kubwa Zaidi: Yesu Kristo, akiwa Mfidi wa wanadamu, ndiye zawadi kubwa zaidi ya zote. Katika kuonyesha ulimwengu wa wanadamu upendo wake mkubwa zaidi, Yehova alimtoa Mwana wake mpendwa na mzaliwa-pekee. (Yn. 3:16) Baraka hiyo isiyostahiliwa kutoka kwa Mungu hustahili kukumbukwa ulimwenguni pote. Lini na jinsi gani? Jioni ya Alhamisi, Aprili 1, 1999, Wakristo ulimwenguni pote watakumbuka Mlo wa Jioni wa Bwana, wakisherehekea Ukumbusho wa dhabihu kubwa kuliko zote.—1 Kor. 11:20, 23-26.
3 Kristo alitufia “tulipokuwa tungali watenda-dhambi,” nasi twaweza kuonyesha shukrani zetu kwa kusherehekea Ukumbusho wa kifo chake na kualika wengine wawepo pamoja nasi katika pindi hiyo ya maana zaidi.—Rom. 5:8.
4 Tukio la Maana Zaidi: Sherehe ya kifo cha Kristo hukazia hasa kwamba alitegemeza enzi kuu ya Mungu bila dosari. Pia yatukumbusha kwamba tunaweza kufurahia msimamo safi mbele za Yehova kwa kudhihirisha imani katika dhabihu ya Yesu, hivyo kuhakikishiwa wokovu. (Mdo. 4:12) Kwa kweli, hili ni tukio la maana zaidi mwakani!
5 Upendo kwa jirani zetu waonyeshwa katika kuwaalika washerehekee Mlo wa Jioni wa Bwana pamoja nasi. Manufaa za fidia zingalipo kwa mamilioni wanaojifunza thamani yake iliyo bora zaidi. (Flp. 3:8) Wale wanaodhihirisha imani katika dhabihu ya Kristo wanaweza kupata tumaini lililo imara la uhai udumuo milele.—Yn. 17:3.
6 Majira ya Ukumbusho huandaa fursa za pekee kwetu kuonyesha uthamini kwa fadhili isiyostahiliwa yenye kuzidi ya Mungu. Huu ni wakati bora kabisa kushiriki kwa bidii katika kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu. Manufaa kubwa zangoja wote wanaofikiria kwa sala zawadi ya bure ya Yehova isiyoweza kufafanuliwa na wanaopanga kuwepo kwenye sherehe ya mwaka huu ya Mlo wa Jioni wa Bwana!