Jinsi Ambavyo Washiriki wa Familia Hushirikiana ili Kushiriki Kikamili—Katika Mikutano ya Kutaniko
1 Familia za Kikristo lazima zitii amri ya kukusanyika pamoja kwenye mikutano ya kutaniko. (Ebr. 10:24, 25) Kwa kushirikiana vizuri, wote wanaweza kufaulu kutayarisha, kuhudhuria, na kushiriki katika mikutano. Hali za familia hutofautiana, lakini kuna mambo ambayo mume Mkristo, mke anayeamini, au mzazi aliye peke yake anaweza kufanya ili kuendeleza umoja wa familia katika mambo ya kiroho, bila kujali idadi ya watoto nyumbani na umri wao mbalimbali.—Mit. 1:8.
2 Tenga Wakati wa Kutayarisha: Washiriki wa familia hushirikiana ili kuona kwamba kila mmoja amejitayarisha vizuri kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. Wengi huchunguza makala ya kila juma ya Funzo la Mnara wa Mlinzi pamoja. Wengine hutayarisha Funzo la Kitabu la Kutaniko au kufanya usomaji wa Biblia wa kila juma wakiwa familia. Lengo huwa ni kuweka mambo makuu akilini kabla ya kuhudhuria mikutano. Kwa njia hiyo, wote watanufaika na yale wanayosikia nao watatayarishwa ifaavyo kushiriki fursa itokeapo.—1 Tim. 4:15.
3 Panga Kushiriki: Kila mtu katika familia apaswa kuwa na mradi wa kutangaza tumaini lake mbele ya wengine kwa kutoa maelezo kwenye mikutano. (Ebr. 10:23) Je, mshiriki wa familia ahitaji msaada au kitia-moyo kufanya hivi? Ni msaada gani ambao kila mtu anahitaji katika kutayarisha migawo ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Wake huthamini waume zao wanapochukua hatua na labda kutoa maoni kuhusu kielezi kinachofaa au kikao chenye kutumika. Wazazi hawahitaji kuhisi kwamba wanapaswa kutayarishia watoto wao sehemu fulani. Kufanya hivyo kutakomesha uwezo wa mtoto kujifanyia mambo mwenyewe. Lakini wazazi wanaweza kusaidia watoto wao na kuwasikiliza wanapojizoeza kwa sauti ya juu.—Efe. 6:4.
4 Panga Kuhudhuria: Watoto wanaweza kufunzwa tangu wakiwa na umri mchanga kuvaa na kuwa tayari kuondoka kwenda mkutanoni kwa wakati uliopangwa. Washiriki wa familia wapaswa kushirikiana katika kushughulikia kazi za kila siku za nyumbani ili wasichelewe.—Ona madokezo katika kitabu Furaha ya Familia, ukurasa wa 112, na kitabu Vijana Huuliza, ukurasa wa 316-317.
5 Wazazi na watoto vilevile wanaweza kuyafikiria kwa makini maneno ya Yoshua wa kale, aliyesema hivi: “Mimi na nyumba yangu tutamtumikia BWANA.” Kisha waazimie kushirikiana ili washiriki kikamili katika mikutano ya kutaniko.—Yos. 24:15.