Zingatia Kazi za Ajabu za Mungu
1 Kwa siku tatu zenye kupendeza, tulikusanyika kwenye Mkusanyiko wa Wilaya wa “Watekelezaji wa Neno la Mungu.” Tuliondoa mawazo yetu kwenye shughuli za kila siku za maisha na kukazia fikira kazi za ajabu za Yehova. Programu hiyo ilikusudiwa kuongeza imani yetu katika Mungu na Neno lake, kuimarisha uhusiano wetu naye, na kuzidisha bidii yetu katika huduma. Twanufaikaje na mambo tuliyofundishwa?—Yn. 13:17.
2 Familia Tiini Neno la Mungu: Mfululizo wa hotuba “Tii Neno la Mungu” ulitusaidia tuchunguze hali ya kiroho ya familia zetu. Watoto wanapenda kujifunza. Kwa hiyo, wazazi wenye kumcha Mungu walitiwa moyo wafanye funzo la Biblia la familia liwe msingi wa kujenga nyumba ya kiroho yenye nguvu. Wengi walio vichwa vya familia wanazungumza pamoja na watoto wao broshua mpya Wewe Unaweza Kuwa Rafiki ya Mungu! Hiyo itawasaidia wasitawishe uhusiano wenye furaha na ulio imara pamoja na Yehova. Wazazi, fundisheni watoto wenu kuzingatia jinsi Mungu anavyohisi. Onyesheni upendo wenu kwake na kwa matendo yake. (Zab. 103:2) Jitahidini pamoja kuweka na kufikia miradi ya kiroho na kujitoa kabisa kumtumikia Yehova.
3 Neno la Mungu Laangaza Njia Yetu: Tulifurahi kupokea kitabu kipya Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote Buku la I. Umefikia wapi katika kusoma buku hili la kwanza? Kitabu cha Isaya chatabiri hukumu zenye kutisha dhidi ya mataifa yasiyomcha Mungu na pia baraka za Ufalme zenye kupendeza kwa watu wa Mungu. (Isa. 34:2; 35:10) Pia chajenga imani na uhakika katika Yehova na njia yake ya kufanya mambo.—Isa. 12:2-5.
4 Unaposoma Unabii wa Isaya Buku la I, unaweza kutambua mara moja jinsi Isaya alivyodumisha uaminifu-maadili kwa Yehova ajapozungukwa na uovu. Alipopewa mwaliko wa kuwa mjumbe wa Mungu, Isaya alijibu hivi: “Mimi hapa, nitume mimi.” (Isa. 6:8) Kutafakari roho yake ya kujitolea kutakutia moyo uendelee kuhubiri habari njema, ukishiriki kikamili kutoa “ushahidi kwa mataifa yote.”—Mt. 24:14.
5 Tukizingatia kazi za Yehova tutautukuza ukuu wake. Kwa hiyo thaminini pendeleo la kuwa watekelezaji wa neno la Mungu!